Patanisho: "Alibeba kila kitu akaniachia mtungi na kikombe moja," Jamaa alalamika

Kimeu aliweka wazi kuwa sio rahisi kurudiana na mke huyo wake wa zamani.

Muhtasari

•Mary alisema ndoa yao ya miaka mitatu ilivunjika takriban miezi miwili iliyopita baada ya yeye kuondoka na kukodi  nyumba nyingine.

•Kimeu  alitaka kujitenga na ujauzito wa Mary huku akidai kuwa  alimuonyesha madharau makubwa hapo awali.

Mtangazaji Gidi
Image: Radio Jambo Instagram

Mwanadada aliyejitambulisha kama Mary Ndunge alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mumewe Stephen Kimeu.

Mary alisema ndoa yao ya miaka mitatu ilivunjika takriban miezi miwili iliyopita baada ya yeye kuondoka na kukodi  nyumba nyingine. Alisema aligura ndoa yao akiwa na ujauzito wa miezi minne baada ya Kimeu kukosa uwajibikaji nyumbani.

"Ilifika mahali hakuwa anatupatia chakula, hakuwa analipa nyumba. Nilikuwa nafanya kazi ya mjengo, ilifika mahali nikalemewa. Tulikuwa tunaishi pamoja ikafika mahali tukaanza kulipa kodi nusu nusu," alisema.

Aliongezeka, "Nilitaka kumuuliza kama ataweza kukodi nyumba kubwa ili tuishi pamoja naye na mtoto wangu. Bado huwa tunaongea na yeye, huwa ananiuliza kilichofanya nitoke kwake." 

Gidi allipopigiwa simu Kimeu aliweka wazi kuwa sio rahisi kurudiana na mke huyo wake wa zamani.

"Kuna kamlima hapo," alisema.

Mary aliomba msamaha na kumsihi mpenzi huyo wake akubali warudiane ili waweze kulea mtoto wao ambaye hajazaliwa pamoja.

Kimeu hata hivyo alitaka kujitenga na ujauzito wa Mary huku akidai kuwa  alimuonyesha madharau makubwa hapo awali.

"Mimba itoke wapi, kwani huwa inatoka kwa hewa?" alihoji.

Aliongeza "Hiyo nimeruka. Vile alinifanyia hapa sioni."

Kimeu alidai kwamba mke huyo wake alimkosea heshima sana wakati alipokuwa akiondoka na hata baada ya kugura.

"Alibeba kila kitu akaniachia mtungi na kikombe moja," alisema.

Aliahidi kumpigia Mary simu ili waweze kusuluhisha mzozo wao kivyao.