Patanisho:Mwanadada akataa usaidizi wa mpenziwe aliyekuwa amekataa kulea mtoto wao

Nyokabi aligura ndoa wakati akiwa mjamzito baada ya mpenziwe kukataa kumhudumia.

Muhtasari

•"Sikuruka mimba. Alienda akanyamaza. Nilikuwa namsaidia kiasi alafu nikaona ameanza kuwa na madharau, ata mimi nikaanza madharau," Mungai alisema.

•Mungai alifichua kwamba amewahi kupiga hatua ya kuenda kwa kina mzazi huyo mwenzake na kumuona mtoto wao.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Samuel Mungai kutoka Nyandarua alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Mary Nyokabi ambaye alikosana naye zaidi ya mwaka mmoja uliopita.

Mungai alisema kuwa Nyokabi aligura ndoa yao wakati akiwa mjamzito baada ya yeye kukataa kumhudumia.

"Sikuruka mimba. Alienda akanyamaza. Nilikuwa namsaidia kiasi alafu nikaona ameanza kuwa na madharau, ata mimi nikaanza madharau. Nilikataa kumsaidia," Mungai alisimulia.

Aliongeza, "Alianza kukataa kuchukua simu na kunitusi. Alienda kwao na akajifungua mtoto wa kike kama mwaka moja uliopita."

Mungai alifichua kuwa mzazi huyo mwenzake amekataa kabisa usaidizi wake sasa licha ya kuwa tayari kusaidia kulea mtoto wao.

"Huwa tunaongea namuuliza kama nimsaidie alafu anasema hataki. Huwa anasema nimpatie muda kama wiki moja, ikipita anaanza madharau tena."

Pia alifichua kwamba amewahi kupiga hatua ya kuenda kwa kina mzazi huyo mwenzake na kumuona mtoto wao.

 "Anafanana na mimi kabisa," alisema.

Nyokabi alipopiga simu alibainisha wazi kwamba hayupo tayari kurudiana na mpenzi huyo wake wa zamani.

"Alikataa kumlea mtoto, alisema ni wake," Alisema.

Nyokabi alimtaka Mungai kumsahau na kutafuta mpenzi mwingine. Hata hivyo alidokeza kuwa bado hajasonga mbele na maisha yake.

Pia alisisitiza kwamba hataki usaidizi wowote kutoka kwa Mungai.

"Kama amesema hivyo ni poa" Mungai alisema.