Patanisho: Mwanadada alia hewani akimuomba nyanyake amuondolee laana ya kutotulia kwenye ndoa

Bibi yake Abigael alilazimika kumtuliza mjukuu wake baada ya kushindwa kuzungumza naye mara moja.

Muhtasari

•Abigael alisema nyanyake alimtamkia maneno ya laana baada ya kukataa kuegemea upande wake na kuegemea upande wa mamake.

•Abigael alipopewa fursa ya kuomba msamaha mwanzoni alishindwa kujieleza na kuangua kilio hewani.

GHOST NA GIDI STUDIONI
GHOST NA GIDI STUDIONI GHOST NA GIDI STUDIONI
Image: RADIO JAMBO

Mwanadada aliyejitambulisha kama Abigael Cheruto ,24, kutoka Eldoret alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na nyanya yake Bi Evelyn ambaye alikosana naye takriban mwongo mmoja uliopita.

Abigael alisema uhusiano wake na nyanya yake uliharibika mwaka wa 2015 wakati mama huyo wa babake alipomtamkia maneno ya laana baada ya kukataa kuegemea upande wake na kuegemea upande wa mamake.

"Tulikosana na shosho 2015. Yeye ni daktari wa dawa za kienyeji,  pia mamangu. Walianza kuvurugana na mamangu waking’ang’ania wateja. Akaanza kuharibia mama sifa kwa wateja wengine. Nikaacha kumuongelesha. Alitaka niliegemee upande wake. Akaleta mvuragano. Hapo akanilaani," Abigael alisimulia.

Aliendelea, "Alisema mpaka nimpigie magoti ndio niolewe. Nilipoolewa alisema ningoje nione kama nitazaa. Nilipozaa akasema tungoje tuone kama nitakaa kwa hiyo ndoa. Baada ya miezi mitatu tukakosana na mume wangu. Nikaolewa tena, kumbe huyo mtu alitaka mtoto tu na sikuwa tayari kupata mtoto. Saa hii niko mwezi wa sita kwa ndoa ya tatu .Nataka kama nilimkosea anisamehe."

Bi Evelyn alipopiga simu alifunguka kuhusu uchungu wake na mjukuu huyo wake akiweka wazi kwamba hana chuki naye.

"Kusema ukweli niliskia uchungu. Kwa boma yangu hatukubahatika kupata shangazi. Nilikuwa nimeweka mpango kwamba wakati itatakikana yeye (Abigael) ndiye atasimama kama shangazi. Na nikaa nikijua hivyo. Sio eti nachukia huyo mtoto. Sijambeba kwa roho yangu. Sijamlaani.  Mwenye makosa ni mama. Yuko mbali na mimi," Bi Evelyn alieleza.

Aliendelea, "Kijana yangu aliaga. Alipoaga huyo mke wake alikuwa ametoka. Nikamtafuta alafu baadae akatoka tena. Nilitaka huyo msichana (Abigael) asome lakini msichana akachukuliwa  tena, baadaye alishindwa kumsomesha. Msichana alifika kidato cha pili, wakampeana kwa jamaa akamuoa. Ile kitu ilifanya nikasirike sana ni meseji aliandikia bibi ya ndugu yake mkubwa. Alimwambia mimi ni roho nyeusi. Uchungu yangu ni yeye kusema mimi ni roho nyeusi."

Abigael alipopewa fursa ya kuomba msamaha mwanzoni alishindwa kujieleza na kuangua kilio hewani. Nyanya yake alipogundua mjukuu wake amezidiwa na hisia alimtuliza na kumhakikishia kuhusu upendo wake kwake.

Baada ya kutulia, Abigael alijitetea akisema, "Nilikwandikia meseji juu ya hasira. Na sipendi vile wewe na mama mnakosana kosana."

Bi Evelyn alimwambia mjukuu wake, "Nilikuwa nataka wewe utafute baraka kutoka kwenu. Wewe ni damu yangu. Asante kwa kukumbuka kuomba msamaha. Chukua huyo mchumba wako mkuje na yeye niwabariki. Ujue mimi ni mama ya babako na uniheshimu. Sijawahi kulaani. Nilisema tu mpaka siku utajua mimi ni nyanyako."

"Wachana na mama yako. Yeye ndiye alibomoa boma yake. Niko na msichana mmoja huyo ndiye najivunia," aliongeza.

Abigael alimwambia nyanyake, "Gogo asante sana kwa sababu ya kunisamehe."

Bi Evelyn alijibu, "Cheru ubarikiwe na utoe hiyo kitu kwa roho eti nimekulaani."