Patanisho: Jamaa aachwa kwa kutoshika simu za mkewe

Muchiri alilalamila kwamba mkewe alikuwa akimshtumu kwa kupuuza simu zake ilhali alikuwa bize kazini.

Muhtasari

•Muchiri alisema mke wake aligura ndoa yao ya mwaka mmoja na miezi mitatu Januari kufuatia ugomvi wa kinyumbani.

•Muchiri aliweka wazi kwamba hakuwa amekosana na mkewe kuhusu jambo linginge lolote.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Jamaa aliyejitambulisha kama Steven Muchiri ,27, kutoka Dagoretti alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Leah Wambura ,22, ambaye alikosana naye hivi majuzi.

Muchiri alisema mke wake aligura ndoa yao ya mwaka mmoja na miezi mitatu Januari kufuatia ugomvi wa kinyumbani.

Alisema mkewe alikuwa akimshtumu kwa kupuuza simu zake, jambo ambalo huenda lilifanya afanye uamuzi wa kutoroka.

"Mimi nikiwa kazi mke wangu alikuwa ananipigia, mara nyingi ilikuwa sipati wakati wa kushika simu juu niko bize," Muchiri alieleza.

Aliongeza, "Nikimpigia anakosa kushika. Wakati akikishika tunabishana naye anasema alinipigia nikikataa kushika. Siku moja vile nilikuja nyumbani nikapata hayuko. Alienda na mtoto wetu. Hayo yalitokea mwezi moja umepita. Sijawahi kuwa na mahusiano mengine, ni kazi tu. Ilifanyika siku mbili, tatu tu."

Wakati alipoulizwa ikiwa amepiga hatua yoyote ya kujaribu kumrejesha mkewe, Muchiri alidai kwamba alienda kwao ila hakupata mtu.

"Nilienda kwao nikapata watu wao ni kama walihama. Sikupata mtu. Nilienda mahali alikuwa amenipeleka, sikupata wazazi wake pale. Sijui mahali mke wangu ako. Ni kama amewashawishi watu wao pia wasinishikie simu juu wakati tuliongea mwisho waliniambia hayuko, lakini mimi najua yuko pale," alisema.

Aidha, aliweka wazi kwamba hakuwa amekosana na mkewe kuhusu jambo linginge lolote.

"Situmii pombe, sigara, muguka... situmii chochote," Muchiri alisema.

Kwa bahati mbaya, ombi la Muchiri la kupatanishwa na mkewe halikufanikiwa kwani simu ya Bi Leah haikuingia.

Alipopewa fursa ya kuzungumza na mzazi huyo mwenzake hewani, Muchiri alimwambia, "Mama Lincoln najua labda tumekuwa tukivurugana juu ya kutoshika simu zako. Wewe jua nakupenda. Wewe rudi nyumbani tulee mtoto. Nakupenda sana mpenzi wangu. Naomba utoe hiyo hasira uko nayo. Unajua nakupenda, sanasana."

Je, ushauri wako kwa Muchiri ni upi?