Patanisho: "Hiyo ujinga sitaki!" Mama Mkwe mkali amshambulia vibaya Ghost kwa kumtafuta bintiye

Brian alisema ndoa yake ilivurugika baada ya wao kuzozana kuhusu mkewe kupanga uzazi bila kumwambia.

Muhtasari

•Brian alidai kwamba mkewe alikuwa akimshtumu kwa kutompenda mtoto wake wa kwanza ambaye alimuoa naye.

•Dadake Mary alibainisha kuwa dada yake tayari ashaolewa kwingine na kumataka Brian amsahau kabisa.

Image: RADIO JAMBO

Jumatatu asubuhi, jamaa aliyejitambulisha kama Brian Oduor kutoka Ugenya alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Mary Munoko  ,24,  ambaye alimuacha hivi majuzi baada kufuatia mzozo wa kinyumbani.

Brian alisema ndoa yake ya miaka mitatu ilivurugika baada ya wao kuzozana kuhusu mkewe kupanga uzazi bila kumwambia.

Pia alidai kwamba mkewe alikuwa akimshtumu kwa kutompenda mtoto wake wa kwanza ambaye alimuoa naye.

"Nimeishi na mke wangu kutoka 2020. Wakati huo nilikuwa Nairobi, alikuwa shule. Alimaliza form 4 akasema anataka tuanze maishi. Wakati huo alikuwa na mtoto mchanga kijana. Alikuwa na mtoto wa miezi minne nikimuoa," Brian alisema.

Aliongeza, "Baadaye tukafanikiwa kupata mtoto naye. Akaanza kusema eti namchukia mtoto wake. Nilimwmabia hakuna kitu kama hiyo nampenda. Mwaka wa 2022, nilimwambia turudi ocha tukae huko."

Brian alisema mzozo uliibuka mapema mwaka huu wakati alitaka wapange jinsi angeenda kujitambulisha kwa wakwe zake.

"Ilifika 2023 nilitaka niende kwao tuweke mambo sawa ikawa maneno mingi. Alichukua mtoto wake akampeleka kwa mama yake alafu akarudi kama ako na family planning. Nikamuuliza mbona anaenda family planning bila kuniambia. Alisema hataki kuzaa tena hadi niende nyumbani kwao," Brian alisema.

Aliendelea, "Tulikosana alafu mama yake akamwambia apande pikipiki aende nyumbani. Dada yake alisema anataka kurudi kukaa na baba mtoto wa kwanza. Aliniachia mtoto wetu wa mwaka mmoja na nusu."

Kwa kuwa Mary hana simu, Brian alitoa namba ya mama yake na ya dada yake.

Wakati mama Mary alipigiwa, alisema, "Hiyo ujinga ya Radio Jambo sitaki!" na kukata simu mara moja.

Dadake Mary alipopigiwa simu alibainisha kuwa dada yake tayari ashaolewa kwingine na kumataka Brian amsahau kabisa.

"Asahau mambo yake," Dadake Mary alisema.

Brian alimwambia, Nilikuwa najaribu kupiga simu haiingi upande wako. Nilikuwa nataka nikuulize mambo ya Mary kwa sababu wewe ni dada yake. Nilitaka kujua kama ni sawa nikuje nyumbani tupange maneno kama tulivyokuwa tumeongea. Ama kama ameamua kuishi na baba mtoto wake."

Dadake Mary alimwambia, "Wewe wakati huo wote ulikaa naye hukuwahi kufikiria kuja nyumbani. Wakati Mary ashakuja ameoleka ndiyo unamtafuta. Mary hayuko sasa na alisema mambo yako hataki kabisa."

Dadake Mary alifunguka mengi zaidi kumhusu Brian akisema, "Mambo iko hivyo vile nimemwambia. Huyo Brayo ako na tabia mbaya. Amekaa na dada yangu miaka mitano hajakuja nyumbani. Wakati dada yangu amepata nafasi akatoroka ndio anamfuatilia nyumbani. Asahau dada yangu tu."

Mwanadada huyo pia alimtaka Brian aache kupost mambo ya familia kwenye ukurasa wake wa Facebook.

Brian alisema amekubali yote yaliyosemwa na kusema atalea mtoto wake pekee yake.

Je, una ushauri gani kwa Brian?