Patanisho: Kijana amlilia babake baada ya kufanya apewe kichapo cha mbwa na wajomba wake

Bw Joseph alifichua kwamba hajawahi kula chakula cha mamake Bramwel tangu mwanawe huyo atoroke nyumbani.

Muhtasari

•Bramwel alisema uhusiano wake na baba yake ulianza kudhoofika mwaka wa 2019 baada ya kumuomba mzazi huyo wake amwonyeshe mahali pa kujenga.

•Bw Joseph alibainisha kuwa hakuwa amemfukuza mwanawe huyo wakati alipoondoka nyumbani kwenda kazini.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Bramwel Simiyu alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na baba yake Joseph Simiyu ambaye alikosana naye kufuatia mzozo wa kinyumbani.

Bramwel alisema uhusiano wake na baba yake ulianza kudhoofika mwaka wa 2019 baada ya kumuomba mzazi huyo wake amwonyeshe mahali pa kujenga.

"Mzozo ulianza kwa mama mdogo. Baba alikuwa amenifukuza akisema mimi sio mtoto wake. Nilikuwa nimenunua mabati kidogo. Kumuuliza mambo ya kujenga, akaniambia hakuna sehemu ya mimi kujenga akanifukuza," Bramwel alisimulia.

Aliongeza, "Nikatoka nyumbani kurudi baadaye nikapata ametumia mabati yangu kujenga nyumba, kumuuliza akaniambia nichunge nyumba sio yangu ni ya kaka yangu. Alisema nitoke na nisirudi."

Bramwel alisema kwamba uhusiano wake na mzazi huyo wake umekuwa mbaya tangu wakati huo na kufichua kwamba familia ilijaribu kusuluhisha baada ya wao kuzozana tena mwaka wa 2021 ila juhudi zikagonga mwamba.

Nilitoka mwaka jana mwezi wa tatu nimekuwa na wasiwasi wa kurudi nyumbani. Hata wajomba walienda nyumbani mmoja akamkata mkono na kisu. Nilikuwa nyumbani mara ya mwisho Machi 2022. Nilitaka nijue msimamo ya baba. Nashindwa nikienda nyumbani nitakaa wapi. Ata nikiwa nyumbani hatakangi tuonane, nakaa na uoga," Bramwel alisema.

Bw Joseph alipopigiwa simu, Bramwel alitumia fursa hiyo kumuomba msamaha na kumsihi warejeshe uhusiano mzuri kati yao.

"Kama nilikukosea naomba msamaha. Naomba turudiane kama mwanzo. Sasa hivi napata shida, pesa nikipata haisaidii. Najuta nilikuongelesha mbaya kama mtoto. Naomba nirudi nyumbani tukae," Bramwel alimlilia babake.

Aliendelea kumweleza jinsi ambavyo amejaribu sana kusuluhisha mzozo wao bila mafanikio.

Bw Joseph alibainisha kuwa hakuwa amemfukuza mwanawe huyo wakati alipoondoka nyumbani kwenda kazini. Aidha, alifichua kwamba kumekuwa na uhusiano mbaya kati yake na mamake Bramwel tangu aondoke.

"Niko tayari kukusamehea. Lakini tutafuata mwenendo wa kimila vile inafaa. Mimi niko tayari kukusamehea mwanangu," Joseph alisema.

Bramwel alimhakikishia mzazi huyo wake kwamba baada ya kukaa chini na kufikiria amejuta mabaya yote ambayo alimtendea.

Kufuatia hayo, Bw Joseph alimwagiza mwanawe apige hatua ya kwenda nyumbani ili wasuluhishe mzozo wao.

"Jipange ukuje nyumbani tukae chini tuongee. Tuite wanafamilia wakuje tujaribu kusuluhisha haya mambo," Bw Joseph alisema.

Bramwel ambaye alisikika kujawa na furaha kufuatia msamaha wa babake alisema ataenda nyumbani mnamo Desemba 3.

"Nimefurahi hata saa hii niko free.. Baba wewe ndiiye tegemeo katika maisha yangu, sina mwingine," Bramwel alisema kwa furaha.