Patanisho: Mwanadada achukua namba ya mpango wa kando wa mumewe na kuiandika kwenye ukuta

Pamela alidai kwamba anafahamu kuhusu mtoto ambaye mumewe alizaa nje ya ndoa.

Muhtasari

•Pamela alisema alitengana na mumewe mwaka wa 2019 baada ya kuwa kwenye ndoa kwa miaka 14.

Pamela pia alidai kuwa anafahamu kuhusu mtoto ambaye mumewe alizaa na mwanamke mwingine nje ya ndoa.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Katika kipindi chetu cha Gidi na Ghost asubuhi, mwanadada aliyejitambulisha kama Pamela alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mume wake John Wanzala.

Pamela alisema alitengana na mumewe mwaka wa 2019 baada ya kuwa kwenye ndoa kwa miaka 14.

Alifichua kuwa uhusiano wake na mumewe ulidhoofika baada ya kumpata na mpango wa kando.

"Tulikuwa tunakaa naye Bungoma town.  Usiku moja simu yake ilipigwa nikaona amesave mtu 'Wife 2'. Ata sikumuuliza, asubuhi niliamka kama nimenuna. Nilichukua hiyo namba nikaandika kwa ukuta. 

Aliniuliza namba ni ya nani nimeandika kwa ukuta, nikamwambia apige. Kupiga ikajiandika 'Wife 2'. Aliondoka tu akaenda. Hatukugombana," Pamela alisema.

Mwanadada huyo alisema kuwa alisalia nyumbani kwa kina mumewe akiwachunga watoto wao watatu licha ya uhusiano wao kuharibika.

Pamela pia alidai kuwa anafahamu kuhusu mtoto ambaye mumewe alizaa na mwanamke mwingine nje ya ndoa.

John alipopigiwa simu alimshutumu mkewe kwa kushinikizwa na kupotoshwa na maneno ya watu.

Pia alipuuzilia madai ya kuwa na mtoto mwingine nje ya ndoa na kudai kwamba mkewe amekuwa akimchunguza sana kwa simu.

"Sina mtoto nje. Ni hao watoto watatu tu ambao wako huko nyumbani. Mimi huwa silewi. Huwa nakuja nyumbani na watoto wanafurahia," John alisema.

Aliongeza, "Shida yake ni kudanganywa sana. Ananichunguza sana kwa simu"

John alikubali kurejesha uhusiano mzuri na mkewe na kumpa masharti ya kutomchunguza na kutoshinikizwa na maneno ya watu.

Pamela alimhakikishia mumewe kuhusu upendo wake mkubwa kwake na kumuomba akatize mahusiano ya nje.