Patanisho: ‘Wrong number’ yazua wasiwasi katika ndoa, jamaa haongei na mkewe lakini chakula anakula

Maryanne alielezea hali ya sasa nyumbani kwake akifichua kumekuwa na wasiwasi mwingi tangu mzozo kutimbuka.

Muhtasari

•Maryanne alifichua kuwa wasiwasi uliingia kwenye ndoa yake ya mwaka mmoja wiki iliyopita wakati mumewe alipomshtumu kwa kuwa na mwanaume mwingine.

•Benson alipopigiwa simu Maryanne alishindwa kabisa kuzungumza naye ili kupatana. Benson hakuwa na budi ila kukata simu.

Image: RADIO JAMBO

Katika kitengo cha Patanisho kwenye Gidi na Ghost asubuhi, Maryanne Nafula (20) alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mume wake Benson Kisaya ambaye hajakuwa na uhusiano mzuri naye katika wiki moja iliyopita.

Maryanne alifichua kuwa wasiwasi uliingia kwenye ndoa yake ya mwaka mmoja wiki iliyopita wakati mumewe alipomshtumu kwa kuwa na mpango wa kando. Alisema ingawa bado wako pamoja, hakuna amani kabisa pale nyumbani.

"Ilikuwa wiki jana. Kuna jamaa mwingine alipiga simu yangu, sijui ilikuwa wrong number. Mume wangu akashuku namcheat. Nikajaribu kumueleza kuwa simjui huyo jamaa akawa haniskii," Maryanne alisimulia.

Aliendelea, "Jamaa huyo allipiga simu akjasema anataka tu kuongea na Joyce, ilhali mimi siitwi hivyo. Nilimpigia kesho yake akasema ilikuwa wrong number. Nilijaribu kumueleza mume wangu akawa haniskii."

Maryanne alielezea hali ya sasa nyumbani kwake akifichua kuwa kumekuwa na wasiwasi mwingi tangu mzozo huo.

"Tunaongeleshana tu kidogo lakini hakuna amani. Chakula anakula tu vizuri. Hata asubuhi amekunywa chai na akaenda kazi. Nimejaribu kumuongelesha lakini hataki. Mimi sina mtu mwingine. Nilijaribu kuambia ndugu yake mkubwa azungumze naye lakini sijui kama wameongea. Aliambia ndugu yake aachane na nyumba yake," alisema Maryanne.

Benson alipopigiwa simu Maryanne alishindwa kabisa kuzungumza naye ili kupatana. Benson hakuwa na budi ila kukata simu.

Gidi hata hivyo alimshauri mwanadada huyo kumwandalia mumewe chakula kizuri na kushiriki naye mazungumzo jioni.

Je, una ushauri upi kwa wawili hao?