"Kidume!" Omanyala ajitapa akionesha tuzo 7 za kifahari alizoshinda kwenye riadha

"Kinachonifanya kuwa mwanadamu kidume si kwa kazi ya mkono wangu bali ya Mungu Mwenyezi maana ndani yake tunaishi," - Omanyala.

Muhtasari

• Mwanariadha huyo alifuzu miezi michache iliyopita kama polisi.

• Ni mshikilishi wa rekodi katika mbio za mita 100 kama mwanamume mwenye mbio zaidi Afrka.

Ferdiand Omanyala, mwanariadha mwenye mbio zaidi Afrika.
Ferdiand Omanyala, mwanariadha mwenye mbio zaidi Afrika.
Image: Instagram

Mwanariadha mwenye mbio Zaidi barani Afrika, Ferdinand Omanyala kwa mara ya kwanza ameonesha tuzo mbalimbali ambazo ameshinda kwenye michezo ya riadha katika miaka miwili iliyopita tangu kujitoma kwenye mwanga wa umaarufu kutokana na mbio zake.

Mwanariadha huyo ambaye pia ni afisa wa polisi ni maarufu kwa kutimuka mbio za mita 100 na 200 na ameweka rekodi kuwa mwanamume wa kwanza Afrika kutimuka mbio za mita mia moja kwa dakika tisa na ushee.

Omanyala alipakia picha kwenye ukurasa wake wa Instagram akiwa nyuma ya safu ya tuzo 7 ambazo amejishindia huku akisema kwamba kuwa mwanamume kamili kunahitaji uzingatifu wa vitu na mambo mengi kwa jumla kabla ya kufikia ushindi.

“Kinachomfanya mwanadamu, sio ushindi anaopata katika mchakato wake wa njia, lakini uwezo wa kukumbatia na kuishi katika maumivu kwa SHUKRANI, nguvu ya kustahimili usumbufu mwingi kwa uwezekano usiojulikana, uimara wa kukaa kwenye njia bila kujali matatizo yanayowakabili,” Omanyala alisema.

Mshindi huyo wa tuzo za Commonwealth mwaka jana katika mbio za mita 100 nchini Uingereza pia alisema ushindi huchangiwa sit u na mazoezi bali kujiamini, ujasiri na Zaidi ya yote kuwa na kibali cha Mwenyezi Mungu.

“Ujasiri wa kufuata bila kuchoka kwa usadikisho mkubwa njia niliochagua. Zaidi ya yote ufahamu na uwezo wa kukiri ukuu niliopewa, si kwa kazi ya mkono wangu bali ya Mungu Mwenyezi maana ndani yake tunaishi, kwa Neema na Upendeleo wake tunastawi, kwa Rehema na Baraka zake tunabarikiwa,” Omanyala aliandika kana kwamba anahubiri.

Umaarufu wa mwanariadha huyo ulianza kuangaziwa katika mashindano ya Olimpiki ya mwaka 2021 nchini Japan lakini hakuweza kuibuka mshindi kwa kukabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa watimukaji wa Marekani.

Mwaka jana pia, katika Mashindano ya Riadha ya Dunia yaliyofanyika Oregon Marekani, mwanariadha huyo hakufana sana, moja ya sababu ya kuvurunda ni matatizo na mahangaiko aliyopitia kupata visa ya kumruhusu kusafiri kwenda Marekani.