Rose Muhando amsamehe msanii wa Kenya Ali Mukhwana kwa tuhuma za kumtapeli

" Bado utabaki kuwa kwangu wewe ni mtoto wa Mungu, hautapungua neno lolote kwangu, nimekusamehe lakini wakati mwingine ukiwa na jambo usifanye maamuzi ukiwa na hasira,”

Muhtasari

• Mchungaji ambaye ndiye mwenyeji wa Muhando pia alisisitiza maneno hayo akikanusha dai la Mukhwana pia kuwa hata yeye alitapeliwa.

Muhando na Mukhwana
Muhando na Mukhwana
Image: Instagram, Facebook

Malkia wa muziki wa injili wa muda mrefu kutoka Tanzania, Rose Muhando ametua nchini Kenya kwa kishindo na kufuta kile ambacho alidai ni uvumi wote ambao umekuwa ukienezwa na msanii Ali Mukhwana kuhusu utapeli.

Mukhwana hivi majuzi alitoa madai mengi dhidi ya Muhando akidai kwamba msanii huyo alimtapeli pesa laki mbili na kukataa kutokea kwenye shoo kama walivyoagana kabla.

Muhando kwa kujibu, alisema kwamba Mukhwana alidanganya kuhusu kiwango cha pesa lakini pia akasisitiza kwamba alirudisha pesa baada ya kushindwa kufika.

“Nimekuja hapa kusema kwamba sio kweli, alinialika na niliposhindwa kwenda kwenye mkutano wa Bungoma, nilirudisha pesa yao. Na hicho kiasi anachosema kwamba ni elfu 200 sio kweli, ni elfu 50 na nilirudisha,” Muhando alisema.

Msanii huyo pia alisema kwamba kwa ameamua kumsamehe Mukhwana kama mtoto wa Mungu wala hatomchukia au kumchukulia hatua zozote za kisheria kwa kujaribu kumchafulia jina.

“Ali nimekusamehe, nimekuachilia, nakupenda kama mtoto wa Mungu, nakupenda sana. Nasema tena nimekuachilia na kukusamehe, na chochote ulichosema nimekusamehe kwa upendo wa Kristo kabisa. Bado utabaki kuwa kwangu wewe ni mtoto wa Mungu, hautapungua neno lolote kwangu, nimekusamehe lakini wakati mwingine ukiwa na jambo usifanye maamuzi ukiwa na hasira,” alisema.

Mchungaji ambaye ndiye mwenyeji wa Muhando pia alisisitiza maneno hayo akikanusha dai la Mukhwana pia kuwa hata yeye alitapeliwa.

Mchungaji huyo alisema kwamba mikutano yote ambayo walikuwa wameratibu na Muhando ilifanyika kama ilivyopangwa kutoka Nairobi hadi Mombasa na kusema huenda Mukhwana alitoa madai hayo kwa hasira.