Nandy afunguka kuhusu malumbano baina yake na msanii wake Yammi, 'ustaa unamsumbua'

Nandy hata hivyo alisema kwamba anamuelewa Yammi kwani katika hatua ambayo amefikia kidogo anahisi kwamba amepata umaarufu kidogo na hivyo kuota pembe lakini akasema watayamaliza.

Muhtasari

• "Bado yupo African Princess! Kupishana inatokea, si unajua bado ni mdogo, halafu u-star ndo unakuja kwa hiyo lazima kuwe na vitu kama hivyo!" Nandy alisema.

Nandy na msanii wake Yammi
Image: INSTAGRAM// THE AFRICAN PRINCESS

Malkia wa Bongo Fleva, Nandy kwa mara ya kwanza amefunguka kuhusu uvumi kwamba yeye na msanii wa lebo yake ya African Princess, Yammi wana malumbano makubwa yanayotishia kuvunjwa kwa mkataba sawia na kile kilichotokea kati ya Diamond na Harmonize 2019.

Akizungumza kwenye media moja ya mitandaoni, Nandy alithibitisha kwamba ni kweli kumekuwa na kutoelewana lakini akasema kwamba si jambo kubwa ambalo linaweza likasababisha ufa baina yao.

Nandy hata hivyo alisema kwamba anamuelewa Yammi kwani katika hatua ambayo amefikia kidogo anahisi kwamba amepata umaarufu kidogo na hivyo kuota pembe katika kile alisema ni ‘ustaa tu ndio unamsumbua’ lakini atajirudi na kujirekebisha.

“Kuhusu Yammi_tz nisingependa kuongelea sana ila tuko sawa! Bado yupo African Princess! Kupishana inatokea, si unajua bado ni mdogo, halafu u-star ndo unakuja kwa hiyo lazima kuwe na vitu kama hivyo! Ukimuangalia Yammi wa mwanzo ni tofauti na wa sasa, mabadiliko ni mengi!” Nandy alisema.

Nandy alianzisha lebo yake mwaka juzi ya African Princess Label na kumsaini Yammi kama msanii wake wa kwanza na ambaye amesalia kuwa pekee miaka miwili baadae.

Wakati anazindua lebo hiyo, Nandy alisema kwamba itakuwa ni lebo tofauti kidogo katika shughuli zake kwani itakuwa inajihusisha na wasanii wa kike pekee.

Nandy alisema kwamba kichocheo kikubwa kuanzisha lebo ya wasanii wa kike pekee ni kuwashika mikono warembo wenye vipaji vya uimbaji kwani alikaa chini na kutathmini hali ya Sanaa nchini Tanzania na kugundua kwamba imetawalia pakubwa na wasanii wa kiume.

Msanii huyo alisema kwamba aliona vipaji vingi vya kike vilikuwa vinatokomea kutokana na kukandamizwa na ubabe wa kiume lakini pia wasanii wa kike kuitishwa rushwa ya ngono kabla ya kusaidiwa kutoboa kisanaa.