Msanii wa Marekani, Usher avutiwa na wimbo mpya wa Nandy, aomba kolabo ya remix

Usher Raymond alimwambia Nandy kwamba wimbo huo umemkosha pakubwa na kumuomba kama anaweza mkubalia wakutane kwa ajili ya kolabo ya remix, huku akimuachia namba yake ya mtandao wa WhatsApp.

Usher Raymond na Nandy
Usher Raymond na Nandy
Image: Instagram

Malkia ya Bongo Fleva, Nandy amevuisha mawasiliano yake ya faragha na msanii wa Marekani Usher Raymond IV ambaye alionesha nia yake ya kufanya kolabo ya remix ya wimbo wa Nandy.

Kwa mujibu wa mawasiliano hayo ambayo Nandy alivujisha kupitia Instagram yake, Usher ndiye alikuwa wa kwanza kumuandikia ujumbe Nandy akimtaarifu kuhusu uzuri na mvuto wa aina yake katika wimbo wake mpya – Dah! – ambao amemshirikisha Alikiba.

Usher Raymond alimwambia Nandy kwamba wimbo huo umemkosha pakubwa na kumuomba kama anaweza mkubalia wakutane kwa ajili ya kolabo ya remix, huku akimuachia namba yake ya mtandao wa WhatsApp kwa mawasiliano ya kina ili kufanikisha kolabo hiyo.

Nandy alionesha furaha yake kutafutwa na mkali huyo wa Marekani na kusema kwamba yuko tayari leo-kesho kufanikisha kolabo hiyo, huku akisema yote ni mipango ya Mungu kwa mwaka 2024.

OOOOOOOOOO🔥 REMIX NO 3 COMING!!!!! I CANT WAIT GOD IS GOOOD OOOOOOH 🙌🏽🙌🏽🙌🏽🙌🏽” Nandy aliandika kwa furaha na mbwembwe.

Wasanii wenzake walimpa hongera lakini baadhi ya mashabiki wakaonekana kumponda kwa kile walisema kwamba angepiga hatua zake kimya kimya mashabiki waje kushtukia wakati tungi limesheheni ubuyu tayari kuumwaya.

Endapo Nandy atafanikisha kolabo hiyo, atakuwa miongoni mwa wasanii wachache wa Bongo ambao wamewahi fanya muziki na wasanii tajika kutoka Marekani.

Wengine ni pamoja na Diamond aliyefanya kolabo na Rick Ross, Harmonize aliyefanya kolabo na Bobby Shmurda.