Msanii nyota wa Tanzania Zuchu aomba radhi kwa onyesho 'lisilofaa'

Onyesho la Zuchu katika kisiwa cha Kendwa cha Zanzibar mwezi uliopita lilijumuisha lugha na ishara za ngono.

Muhtasari

• Taasisi ya Sanaa, Sensa, Filamu na Utamaduni Zanzibar Jumanne ilisema kuwa maonyesho hayo yalikwenda kinyume na mila, desturi na utamaduni wa visiwa hivyo.

Mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 30 ni mmoja wa wanamuziki wakubwa Afrika Mashariki
Mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 30 ni mmoja wa wanamuziki wakubwa Afrika Mashariki
Image: HISANI

Mwimbaji maarufu wa Tanzania Zuchu ameomba radhi baada ya mamlaka visiwani Zanzibar kumsimamisha kwa muda wa miezi sita kujihusisha na shughuli zote za kisanii katika visiwa hivyo kutokana na onyesho ambalo waliona kuwa halifai kimaadili ya eneo hilo.

Onyesho la Zuchu katika kisiwa cha Kendwa cha Zanzibar mwezi uliopita lilijumuisha lugha na ishara za ngono.

Taasisi ya Sanaa, Sensa, Filamu na Utamaduni Zanzibar Jumanne ilisema kuwa maonyesho hayo yalikwenda kinyume na mila, desturi na utamaduni wa visiwa hivyo.

Pia ilimtaka Zuchu kuomba msamaha wa maandishi.

Katika video iliyosambazwa kwenye Instagram yake Jumanne jioni, mwanamuziki huyo aliomba msamaha kwa kosa lolote lililosababishwa na uchezaji wake.

"Lengo lilikuwa kuburudisha na sio kupotosha," alisema.

Mwimbaji huyo pia amesimamishwa "kujishughulisha na shughuli zozote za kisanii" Zanzibar kwa muda wa miezi sita ijayo na baraza la utamaduni la eneo hilo.

Zuchu, jina halisi Zuhura Othman Soud, ni mmoja wa wanamuziki waliofanikiwa zaidi Afrika Mashariki.

Mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 30 ndiye mwanamuziki wa kwanza wa kike katika Afrika Mashariki kupata wafuasi milioni moja katika mtandao wa YouTube, kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Yeye pia ni mwanamuziki wa kwanza wa kike Afrika Mashariki na ni msanii wa tano pekee wa kike barani humo kuzidi mara milioni 500 kutazamwa kwenye YouTube, kulingana na lebo yake ya WCB Wasafi.