Bien amjibu Otile kwa kudai hakuna wasanii wa kimataifa Kenya

Nimekuwa kwenye ziara mwaka mzima nje ya nchi; Nimecheza Kenya mara moja mwaka huu

Muhtasari

•Inanikera kidogo Otile anaposema hivyo kwa sababu watu wana shughuli nyingi za kujenga, na ninaweza kuelewa anaposema hivyo kwa sababu hajawahi kwenda upande mwingine.

Bien na Otile
Image: Instagram

Msanii kutoka Kenya Bien Aime Baraza amejibu madai ya Otile Brown, kwa kusema kwamba hakuna wasanii wa kimataifa nchini Kenya.

Bien ambaye alikuwa kwenye  Obinna TV alimtaka Otile Brown kufikiria na kutafakari upya maneno yake kwa sababu kuna wasanii wengi maarufu wa Kenya ambao sio tu wanafanya vizuri kimuziki bali pia kuwaangusha wasanii wa kimataifa anaowazungumzia.

“Inanikera kidogo Otile anaposema hivyo kwa sababu watu wana shughuli nyingi za kujenga, na ninaweza kuelewa anaposema hivyo kwa sababu hajawahi kwenda upande mwingine.

Sofia Nzau ni nani kwako? Hujawahi sikia Mwaki? Ina views milioni 100 kwenye Spotify, na hata aliperform nchini Afrika Kusini.

Je, yeye si msanii wa kimataifa? Tumesikia wasanii wa kimataifa huko nyuma pia. Wimbo mkubwa wa Kiswahili ni ‘Jambo Bwana,uliimbwa miaka mingi iliyopita.” Bien alieleza.

Kulingana na Bien, Otile anaonesha kile anachohisi, na hawezi kulinganishwa naye, kwa sababu alichofanya ni zaidi yake.

“Nimekuwa kwenye ziara mwaka mzima nje ya nchi, nimecheza Kenya mara moja mwaka huu, nimecheza zaidi ya maonyesho 20.

Nimekuwa nikitembelea na kuuza kila mahali. Nimetembelea sehemu za Uropa na Australia, kwa hivyo sijui Otile anafafanua nini kama msanii wa kimataifa." Bien alisema.