Star Chebet atoa taarifa ya kutia wasiwasi kuhusu maisha yake "Nilijiingiza kwenye mambo yasiyofaa!"

Alikiri kuingizwa katika mambo ambayo hakuwahi kutarajia na akasema ameshuhudia matokeo yasiyoeleweka.

Muhtasari

•Ameeleza wasiwasi wake kuhusu hatima yake akisema aliingia katika mambo ya kutisha baada ya kufanya urafiki na watu waliofuata njia tofauti.

•“Niko njiani kuelekea Nakuru na gari inasonga.., Hisia zangu zinaonyesha sitakuwa sawa," Chebet alisema.

Image: INSTAGRAM// STAR CHEBET

Wasiwasi umeibuliwa baada ya jumbe za kutatanisha kuchapishwa kwenye akaunti rasmi ya Instagram ya muigizaji maarufu wa Kenya, Star Chebet almaarufu Matilda.

Katika posti za Alhamisi asubuhi, muigizaji huyo wa zamani wa kipindi cha Real Househelps of Kawangware alizungumza kuhusu yeye kujiingiza katika mambo yasiyofaa.

Ameeleza wasiwasi wake kuhusu hatima yake akisema aliingia katika mambo ya kutisha baada ya kufanya urafiki na watu waliofuata njia tofauti.

“Haya jamani, nimekua kitambo tangu nipost hapa, lakini maisha yamekuwa yakienda kasi sana... sijui mwisho wa siku nitakuwa sawa, lakini nilijiingiza kwenye kitu ambacho siwezi kukirudisha nyuma. Maisha ni ya kiroho; Nadhani nilijiingiza kwenye uhalisia usio sahihi katika utafutaji wangu wa amani ya akili na kuingia katika nguvu zisizo sahihi,” Star Chebet alisema katika mojawapo ya machapisho yake.

Chebet aliendelea kuomba msamaha kwa watu ambao huenda amewakosea na pia akatoa shukrani kwa watu ambao wamemuonyesha sapoti.

“Nilipata marafiki wapya ambao walikuwa katika njia tofauti kabisa na nikaingia katika mambo ambayo sikuyatarajia. Na sidhani itaisha poa. Marafiki wa Tiktok *** na marafiki zenu poleni sana,” alisema.

Katika chapisho lingine, muigizaji huyo mrembo alizungumza kuhusu kuingizwa katika mambo ambayo hakuwahi kutarajia na matokeo ambayo hakuelewa kutokea baadaye.

"Nilitumika kufungua portal kwenye mto Kimugu huko Kericho na nikaingizwa kwenye mambo ambayo sikulitarajia.. Sikujua ni nini kilikuwa kinatokea hadi kikatokea. Maisha ni ya kiroho na roho huingia kwenye mizozo bila kujua wakati mwingine,” Chebet alisimulia.

Aliongeza, “Niko njiani kuelekea Nakuru na gari inasonga.., Hisia zangu zinaonyesha sitakuwa sawa.”.

Watumiaji wa mitandao ya kijamii ambao wameona machapisho ya Chebet wameelezea wasiwasi wao huku wengine hata wakitafuta njia za kuwasiliana naye.

 

Chebet alijipatia umaarufu kufuatia uhusika wake katika kipindi cha ‘The Real Househelps of Kawangware'. Alicheza kama msichana aliyejulikana kama 'Matilda'