Chicago Marathon: Mkenya Brigid Kosgei avunja rekodi ya ulimwengu

Brigid Kosgei-compressed
Brigid Kosgei-compressed
Ilikuwa wikendi ya kihistoria kwa Wakenya  baada ya mwanariadha mwingine Brigid Kosgei  kuvunja rekodi ya ulimwengu  katika mbio  za wanawake za masafa marefu siku Jumapili mjini Chicago.

Rekodi ya awali ya mbio hizo ilikuwa ikishikiliwa na Paula Radcliffe  kwa kipindi cha miaka 16  iliyopita.

Kosgei  alijizatiti na akamaliza katika muda wa 2:14:04, zaidi ya dakika sita mbele ya Ababel Yeshaneh, ambaye alikimbia masaa mawili, dakika 20 na sekunde 51, na Gelete Burka ambaye alikimbia masaa mawili, dakika 20 na sekunde 55 wakati Ethiopia ilimaliza katika nafasi ya pili na tatu.

Mwanariadha huyu  mwenye umri wa miaka 25 alishinda kwa mara ya kwanza katika mashindano ya London maratahon mapema mwaka huu, na sasa ameshinda kwa mara ya  tatu baada ya ushindi huko Chicago mwaka 2018.

Kosgei alipongezwa na Radcliffe baada ya kunyakua taji hilo la bingwa wa dunia katika mbio za masafa marefu kwa kina dada.

Rekodi iliyovunjwa na Brigid Kosgei ilithibitishwa na  shirika la IAAF kwa kuwa alikimbia katika madhari ya mashindano yaliyo rasmi kinyume na mbio za Kipchoge ambapo hapakuwa na mshindani na alisaidiwa na wanariadha wengine  41 kufanikisha mbio hizo.

Alimaliza wikendi ya kupendeza  katika fani ya riadha Jumapili baada ya Eliud Kipchoge kutawazwa   mwanariadha wa kwanza duniani kukimbia mbio za kilomita 42 chini ya saa mbili.