Uganda yapinga uwepo wa hukumu ya Kifo

Bunge la Uganda limepitisha sheria inayopinga hukumu ya adhabu ya kifo kwa baadhi ya uhalifu, na kufanya marekebisho katika sheria nne tofauti ikiwemo sheria ya kupambana na ugaidi.

Kama sheria hiyo itasainiwa na rais Yoweri Museveni , marekebisho hayo yatasitisha hukumu ya kifo kwa uhalifu mkubwa zaidi, kwa maelekezo ya jaji.Watunga sheria wanasema kuwa hii ni hatua kubwa inayoweza kutokomeza hukumu hiyo, jambo ambalo mahakama iliwahi kupigia kelele.

Kuna wafungwa 133 ambao wamehukumiwa kunyongwa lakini sasa imepita miaka 20 tangu wahukumiwe.Kumekuwa na kampeni mbalimali za kutokomeza hukumu hilo, kufuatia hukumu ya mwaka 2009 ya mfungwa Susan Kigula ambaye alihoji juu ya hukumu ya kifo kuwa kinyume na katiba.

Mahakama baadae ilitaka hukumu ya kifo isiwe lazima kwa kesi za mauaji, na kuwasisitiza watu kuwa mtu hapaswi kuwekwa jela kwa miaka mitatu wakati amehukumiwa kunyongwa muda huo ukipita mfungwa huyo ni sawa kuwa amepewa hukumu ya kifungo cha maisha.

Mara ya mwisho Museveni kudihinisha hukumu ya kifo itekelezwe ilikuwa mwaka 1999 kwa watu 27 katika gereza la Luzira hapa mjini Kampala.

Kadhalika, aliidhinisha mahakama ya kijeshi kutekeleza hukumu ya kifo mwaka 2005.

Makubaliano ya kusitisha sera au utekelezaji

Ripoti ya katibu mkuu wa Umoja wa mataifa kuhusu hukumu ya kifo imewasilishwa katika tume ya haki za binadamu mwezi Septemba mwaka huu na kusema kuwa kuna mataifa 170 wameachana na adhabu hiyo ya kifo kisheria na utekelezaji au hajauliwa mtu kwa zaidi ya miaka 10.

Umoja wa mataifa ambayo ina wanachama 193, hivyo ni mataifa 23 tu ndio ambayo inawezekana walitoa hata hukumu moja ya kifo katika muongo uliopita.

Kwa kihistoria, Kanisa limekuwa likizuia adhabu ya kifo, ikiwa ni pamoja na katika karne ya 20.

Hukumu ya kifo Afrika mashariki

Nchini Kenya wahalifu wamekuwa wakihukumiwa kifo Kenya lakini hakuna aliyewahi kuuawa tangu miaka ya 1980.Watetezi wa haki wamekuwa wakipigania kuondolewa kwa hukumu hiyo.Baadhi ya wafungwa hata hivyo wamekuwa wakilalamika kwamba hakuna tofauti ya hukumu ya kifo na maisha jela kwani mfungwa huwa anaishi jela hadi kifo chake.

Nchini Tanzania, takriban wafungwa 500 wapo katika jela za Tanzania wanakabiliwa na hukumu hiyo.Rais wa Tanzania, John Magufuli amekwisha weka wazi msimamo wake juu ya utekelezaji wa hukumu ya kifo kuwa hawezi kusaini mfungwa yeyote aliyehukumiwa adhabu hiyo kwenda kunyongwa.

Mara ya mwisho kwa mfungwa kunyongwa nchini ilikuwa mwaka 1994, enzi za utawala wa Rais wa awamu ya pili wa nchi hiyo, Ally Hassan Mwinyi.