Nitakabiliana na yeyote anayejihusisha na ufisadi: Ruto awaonya wafanyikazi wa serikali

Pia alisisitiza kuwa ufisadi utaharibu mpango huo unaolenga kubuni nafasi za kazi na kuwajengea Wakenya nyumba za bei nafuu.

Muhtasari
  • Zaidi ya hayo, watatakiwa kulipa faini ya lazima ambayo ni mara mbili ya fedha ambazo zimetumika vibaya.
Rais William Ruto aidhinisha Mswada wa Fedha wa 2023 Ikulu Juni 26, 2023.
Rais William Ruto aidhinisha Mswada wa Fedha wa 2023 Ikulu Juni 26, 2023.
Image: PCS

Rais willian Ruto amewaonya wafanyikazi wa serikali kuhusu athari mbaya iwapo kashfa za ufisadi zitaibuka katika mpango wa ujenzi wa nyumba za bei nafuu.

Akizungumza wakati wa kutiwa saini kwa mswada wa ujenzi wa nyumba kuwa sheria katika Ikulu ya Nairobi mnamo Jumanne, Machi 19, mkuu wa nchi alisisitiza kwamba hataunga mkono aina yoyote ya ufisadi akitaja hatua alizoweka kuzuia visa kama hivyo.

Ruto alifichua kuwa serikali tayari imekubaliana kuhusu bei ya vifaa vya ujenzi, akisisitiza kwamba hakutakuwa na kesi za kuongezwa kwa bei.

Kwa upande mwingine, alieleza kuwa ufisadi hauwezi kuruhusiwa katika mpango huo ikizingatiwa kuwa Wakenya walikuwa wakifanya michango ya kila mwezi.

Pia alisisitiza kuwa ufisadi utaharibu mpango huo unaolenga kubuni nafasi za kazi na kuwajengea Wakenya nyumba za bei nafuu.

"Nataka niwahakikishie kuwa nitafanya lolote litakalohitajika ili kukabiliana na yeyote anayejihusisha na ufisadi. Nitalinda rasilimali hizi kwa ajili ya maendeleo ya watu wa Kenya."

"Ninataka kutoa onyo kwa mtu yeyote anayetoka nje ya mtandao, haitakuwa biashara kama kawaida. Mpango huu hautakuwa na rushwa. Tumekubaliana juu ya kiasi na gharama",  alisema rais.

Sheria ya nyumba za bei nafuu inabainisha kuwa mtu yeyote ambaye atashiriki katika matumizi mabaya ya fedha katika mpango huo atatozwa faini ya ksh. milioni 10.

Zaidi ya hayo, watatakiwa kulipa faini ya lazima ambayo ni mara mbili ya fedha ambazo zimetumika vibaya.

Aliyasema hayo baada ya mwanakandarasi mwanamke kulalamika kuwa hakuna vyumba vya kubadilishia nguo vya wanawake.

Aliwataka Wakenya kuunga mkono mpango huo ambao alidokeza kuwa unalenga kubuni nafasi za kazi kwa vijana na kutokomeza makazi duni.

"Ahadi yangu ni kwamba katika miaka 10 ijayo hatutakuwa na makazi duni Kibra, tutakuwa na shamba. Tunapounda kitengo cha makazi tutahamisha watu kuishi humo",Ruto alisema.