Museveni awaomba Wakenya msamaha, ataja sababu za kumpandisha cheo mwanawe Muhoozi

Museveni alisema si sahihi kwa mwanawe kutoa matamshi ya aina hiyo.

Muhtasari

•Jumbe za Muhoozi zilizua taharuki iliyomfanya rais Museveni kuwa chini ya shinikizo kubwa la kuomba radhi.

KWA HISANI
KWA HISANI
Image: Muhoozi Kainerugaba

Rais wa Uganda Yoweri Museveni ameeleza  sababu za kumpandisha cheo katika jeshi mwanawe wa kwanza huku akiomba msamaha kwa Wakenya kufuatia matamshi yake ya kudhalilisha Kenya.

Muhoozi Kainerugaba, kamanda wa zamani wa Jeshi la nchi kavu la Uganda alipandishwa cheo na kuwa Jenerali kamili baada ya kudai kuwa anaweza kuteka jiji kuu la Kenya, Nairobi chini ya wiki mbili.

Jumbe za Muhoozi zilizua taharuki iliyomfanya rais Museveni kuwa chini ya shinikizo kubwa la kuomba radhi.

"Ninasikitika sana kwa alichofanya mwanangu Muhoozi, rais wa Uganda ameomba msamaha kutokana na tweets za kutisha ambazo mwanawe alichapisha kwenye mitandao ya kijamii," alisema.

"Nawaomba kaka na dada zetu wa Kenya watusamehe kwa tweets zilizotumwa na Jenerali Muhoozi, Kamanda wa zamani."

Museveni alisema si sahihi kwa mwanawe kutoa matamshi ya aina hiyo.

"Si sahihi kwa maafisa wa Umma, wawe wa kiraia au wa kijeshi, kutoa maoni au kuingilia kwa njia yoyote, katika masuala ya ndani ya nchi ndugu," alisema.

"Jukwaa la pekee lililo halali ni Mfumo wa Mapitio ya Rika wa Umoja wa Afrika au mazungumzo ya siri kati yetu au EAC na AU kwa maoni ya umma."

Museveni alieleza zaidi kwa nini alimpandisha cheo mwanawe kuwa jenerali kamili.

“Hii ni kwa sababu kosa hili ni kipengele kimojatu mbapo ametenda vibaya kama afisa wa Umma. Walakini, kuna michango mingine mingi mizuri ambayo Jenerali ametoa na bado anaweza kutoa, "alisema.

Aliongeza, "Hii ni njia iliyojaribiwa kwa muda ili kusitisha mabaya na kuongeza nguvu mazuri. Poleni sana ndugu zetu Wakenya."