Sakaja amjibu Nyong'o kuharamisha maandamao Kisumu kuja kuyafanya Nairobi

Sakaja pia alisema kuwa yapo makubaliano kwamba hakuna maandamano na vurugu zaidi zitaruhusiwa jijini Nairobi.

Muhtasari

• Gavana Sakaja alisema kwamba kwa nia njema ya ugatuzi, angependa kumuomba Nyong’o kutoleta maandamano ya Kisumu Nairobi

Gavana Sakaja amjibu Nyong'o kuhusu kuleta maandamano Nairobi.
Gavana Sakaja amjibu Nyong'o kuhusu kuleta maandamano Nairobi.
Image: Facebook

Saa chache baada ya gavana wa Kisumu profesa Anyang’ Nyong’o kutangaza marufuku ya kufanyika kwa maandamano katika kaunti hiyo na badala yake kuungana na vigogo wa Azimio kuandamana Nairobi, gavana wa jiji kuu Johnson Sakaja amejibu mipigo.

Katiba barua hiyo ambayo Sakaja aliipa mada ya “rudi kwa mtumaji” alisema kwamba kitendo cha Nyong’o kupiga marufuku maandamano katika kaunti yake na kuyapeleka Nairobi ni kitendo cha udhalilishaji na kusema kwamba amekuwa akifanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kwamba wakaazi wa Nairobi wanapata huduma nzuri katika mazingira tulivu ya Amani na usalama.

“Hatua ya gavana wa Kisumu kufunga maandamano na vurugu huko na kuyaleta Nairobi ni dhihaka na haitokubalika kabisa. Kaunti ya Nairobi tayari imekuwa mwenyeji wa maandamano hayo mara mbili, na tumeona madhara yake. Watu wa Nairobi wamevumilia vurugu hizo na kipato chao kimepotea kutokana na hilo,” sehemu ya barua ya Sakaja ilisoma.

 Gavana Sakaja alisema kwamba kwa nia njema ya ugatuzi, angependa kumuomba Nyong’o kutoleta maandamano ya Kisumu Nairobi na badala yake kuyafanyia huko huko, akisema kwamba Nairobi tayari washashiba na hasara zake.

“Tumekubaliana kwamba hakuan maandamano Zaidi ambayo yatapewa ruhusa jijini Nairobi. Nairobi ni kitovu cha kiuchumi kwa nchi nzima na ukanda huu, uongozi wangu unafanya kazi kwa juhudi kubwa kuhakikisha kwamba huduma zinatolewa sit u kwa wana Nairobi bali kwa taifa zima, ndio maana tulihakikisha kuweka usalama wa watu na wanyama,” Sakaja alimfokea Nyong’o.