•Musa Ogendo Sirangi hakujibu shtaka hilo baada ya mahakama kuahirisha kesi hiyo hadi Jumatatu wiki ijayo.
Mwanamume aliyedaiwa kuiba kompyuta ya mkononi ya thamani ya Sh 220,000 kutoka kwa IEBC Jumatano wiki hii alifikishwa katika mahakama ya Nairobi kujibu shtaka la wizi.
Hata hivyo, Musa Ogendo Sirangi hakujibu shtaka hilo baada ya mahakama kuahirisha kesi hiyo hadi Jumatatu wiki ijayo.
Hii ni baada ya Sirangi kumweleza Hakimu Ondieki kuwa alivamiwa na polisi alipokamatwa na hakuwa na wakili.
Katika shtaka lililowasilishwa kortini, inadaiwa kuwa mnamo Agosti 17 katika jumba la Anniversary Towers kando ya chuo kikuu jijini Nairobi, aliiba kompyuta ndogo aina ya HP Probook ya thamani ya Sh 226,240 mali ya IEBC.
Sirangi atazuiliwa katika kituo cha Polisi cha Central hadi Jumatatu atakaposhtakiwa rasmi kwa kosa hilo.