- Watu wengi wamefanya shindano la kuucheza wimbo huo
- Kote duniani wimbo huo umetawala kumbi zote za video na densi
Kiongozi wa walio wengi bungeni Amos Kimunya na mwenzake wa walio wachache John Mbadi siku ya jumatano wamewaongoza wabunge kufanya densi ya wimbo maarufu wa Jerusalema.
Wabunge waliunda foleni mbili sako kwa bako ili kuifanya densi hiyo katika majengo ya bunge huku wakijaribu kufuata mfano wa miondoko na unenguaji ambao maelfu ya watu wamefanya kote duniani tangu shindano hilo la kudensi kuanza.
Kimunya na Mbadi waliwasisimua wenzao kwa weledi wao kufanya densi hiyo huku wakishangiliwa .
Wabunge wamekuwa wakifanya mazoezi ya kuweza kufanikisha densi hiyo kwa siku mbili. Kimunya amesema ni muhimu kwa viongozi pia kuwa sehemu ya vugu vugu kama hilo la kijamii wakati huu mgumu.
Wimbo wa Jerusalema umepigwa jeki na idhinisho kutoka kwa marais, makasisi na makundi mbali mbali ya watu, vikosi vya usalama na hata kampuni nyingi kote duniani.