DJ Joe Mfalme avunja kimya kabla ya kufikishwa mahakamani leo, Aprili 8

Meneja wake amesema wanatarajia matokeo ya uchunguzi wa polisi wakati wa kikao cha mahakama.

Muhtasari

•Joe Mfalme atafikishwa mahakamani kwa mara ya pili mwendo wa saa tatu alfajiri kuhusiana na madai ya shambulio la mpelelezi Felix Kelian.

•Meneja wa Joe Mfalme pia hakukosa kutuma risala za rambirambi kwa familia ya marehemu Kelian.

DJ JOE MFALME akiwa kizimbani na wenzake
DJ JOE MFALME akiwa kizimbani na wenzake
Image: DOUGLAS OKIDDY

Mcheza santuri maarufu wa Kenya Joseph Mwenda Munoru almaarufu DJ Joe Mfalme anatarajiwa kufikishwa katika Mahakama ya Kibera leo, Jumatatu, Aprili 8.

Joe Mfalme atafikishwa mahakamani kwa mara ya pili mwendo wa saa tatu alfajiri kuhusiana na madai ya shambulio la mpelelezi wa kituo cha polisi cha Kabete, Felix Kelian.

Akizungumzia hilo, mtumbuizaji huyo ambaye amekuwa rumande kwa wiki mbili zilizopita, kupitia kwa meneja wake alisema wanatarajia matokeo ya uchunguzi wa polisi wakati wa kikao cha mahakama.

"Siku 14 zilizopita zimekuwa kali, lakini jumbe zenu za mshikamano na ziara zimeifanya timu kuendelea. DJ Joe Mfalme na timu watarejea katika Mahakama ya Kibera kesho, Jumatatu tarehe 8 ili kusikiliza matokeo ya uchunguzi,” Innocent Bernd, meneja wa DJ huyo alisema katika taarifa iliyotolewa Jumapili jioni.

Aliongeza, “Mahakama inaanza saa tatu asubuhi. Tutatoa taarifa mara tu tutakapomalizana na mahakama kesho. Asanteni kwa kusimama na timu."

Meneja wa Joe Mfalme pia hakukosa kutuma risala za rambirambi kwa familia ya marehemu Kelian.

"Tunataka kutoa shukrani zetu za dhati kwa uaminifu wenu usioyumba na kutia moyo katika kipindi hiki kigumu. Mawazo na sala zetu bado ziko kwa familia na marafiki wa walioathiriwa na mkasa huo,” Bernd alisema.

Joe Mfalme na timu yake walifikishwa katika Mahakama ya Kibera kwa mara ya kwanza mnamo Machi 25, 2024 kuhusiana na madai ya kifo cha Felix Kelian.

Kisha mahakama iliruhusu ombi la polisi kumzuilia mtumbuizaji huyo na wengine sita kusubiri uchunguzi zaidi kuhusu kesi hiyo.

Hakimu Margret Murage alisema washukiwa hao wangezuiliwa kwa siku 14.

DCI ilikuwa imeomba siku 21 lakini mahakama ilisema siku 14 zitatosha.

Mtumbuizaji huyo alizuiliwa katika kituo cha polisi cha Muthangari pamoja na Eric Gathua na Simon Wanjiru.