Harambee Stars kukabana na Msumbiji leo, Kasarani

Harambee Stars watakabana na Msumbiji katika mechi ya kirafiki alasiri ya leo uwanjani Kasarani, kujitayarisha kwa michuano ya kufuzu kwa AFCON mwaka wa 2021.

Nahodha Victor Wanyama atacheza huku Farouk Shikhalo huenda akaanza kama kipa kwani Patrick Matasi hayuko. Kocha mkuu Francis Kimanzi anasema wachezaji hao ambao wamekuwa kambini kwa siku tano, wako katika hali nzuri na atawabadilisha ili kujaribu wachezaji wapya.

Mechi hiyo inaanza saa kumi kamili huku tikiti zikiuzwa kwa shiilingi 200.

Hayo yakijiri, timu ya raga ya kinadada Kenya Lionesses itakabana na Zimababwe katika michuano ya kufuzu kwa Olimpiki ya raga ya wachezaji 7 saa sita mchana baada ya kuongoza kundi A na rekodi ya kutoshindwa.

Kinadada hao waliwacharaza Ghana 36-0, baada ua kuwanyuka Botswana 51-0 na Senegal 36-0. Kenya iliorodheshwa ya kwanza na jumla ya alama 121.

Tukielekea ulaya, Nemanja Matic huenda akajumuika tena na kocha Antonio Conte, iwapo Inter Milan itajaribu kumsajili kiungo huyo wa kati msimu huu, kutoka Manchester United.

Mchezaji huyo wa umri wa miaka 31 raia wa Serbia amecheza mara tatu katika ligi ya Primia msimu huu, tangu kuteuliwa kwa Ole Gunnar Solskjaer. Matic alichezea Chelsea kwa miaka mitatu, msimu wa mwisho chini ya Antonio Conte kabla ya kujiunga na United kinyume na alivyotaka Conte Agosti mwaka 2017.

Italia waliwanyuka Ugiriki 2-0 na kufuzu kwa fainali ya michuano ya Uro mwaka 2020. Baada ya kutoka sare tasa katika kipindi cha kwanza Jorginho waliwaeka mbele kupitia kwa bao kunako dakika ya 63 kabla ya Federico Bernadeschi kufunga la pili.

Wakati huo huo Uhispania ilikaribia kufuzu kwa michuano hiyo walipotoka sare ya 1-1 na Norway.