Kipchoge aliwasili nchini bila mapokezi ya kitaifa na sherehe mnamo Jumatano asubuhi.
Kinyume na vile ilivyotarajiwa, Wakenya walitamani sana kupewa fursa ya kumuenzi bingwa huyu wa riadha. Hata baadhi wakitaka sikukuu kutengwa kwa ajili yake, lakini Kipchoge anasema: "Sitasherehekea kwa kuchinja ng'ombe. Hayo hayatawaHifanyika katika maisha yangu. Sherehe yangu kubwa huishia uwanjani ninapokata utepe"
Anatarajiwa kupokelewa pamoja na familia yake na timu yake katika kambi yake na mazoezi Global Communications.
"Kwa sasa tunapanga mikakati ya kusherehekea. Ni vizuri kusherekea ushindi, kutulia, kupongeza timu yangu na kujiandaa kwa shughuli zijazo," Kipchoge alisema.
Hata hivyo bingwa huyu alifutilia mbali wito wa kufanyiwa sherehe za kitaifa.
"Nitasherehekea bali kimya kimya. Kwa njia ya unyamavu, sio kwa kishindo" Kipchoge alisema.
Hata hivyo Kipchoge hakutoa maazimio yake iwapo atashiriki katika michezo ya Olimpiki jijini Tokyo Japan mwaka ujao.
Alisema kwamba ingali mapema kusema hatua yake ijayo.
"Sitaki kuzungumzia mashindano ya Tokyo sasa, lakini natumai nitakuwa katika mstari wa kuanzia. Bado ninayo miezi kadhaa kabla ya Tokyo na ninahitaji kusherekea mwanzo." alisema.
"Ninawapongeza wakenya wote walionishabikia kwa muda huo wote wa 1:59:40. Ninawaambia wajipe motisha na wajue kwamba binadamu hadhibitiki akiamua kutenda" Kipchoge alisema.