Mashabiki wa Chelsea watoa msaada wa chakula kwa wafungwa gerezani Machakos

Mashabiki hao walibeba vyakula kama unga na mafuta ya kupika kama zawadi ya kuonesha upenda kwa wafungwa msimu huu wa Valentino.

Muhtasari

• Mashabiki wa Chelsea walisema wana matawi sehemu mbalimbali kama Kisii, Nairobi, Meru na sehemu zingine.

Mashabiki wa Chelsea wakitoa chakula Machakos
Mashabiki wa Chelsea wakitoa chakula Machakos
Image: Screengrab

Kikundi cha mashabiki wa Chelsea nchini Kenya kimefanya kitendo cha faraja baada ya kutoa msaada wa chakula na bidhaa zingine kwa wafungwa wa kike na kiume katika gereza la Machakos.

Kikundi hicho walifika katika gereza la Machakos wakiwa na bidhaa mbali mbali zikiwemo mafuta ya kupika na unga, huku wamevalia jezi ya timu hiyo kutoka Uingereza na kuwakabidhi wafungwa kama njia moja ya kuwaonesha upendo siku moja kabla ya siku ya wapendanao ya Valentino.

Kundi hili limekuwa likifanya mitikasi yao kwenye mitandao ya kijamii na safari hii waliamua kutia tabasamu kwenye nyuso za wafungwa hao kimwili ili pia wajihisi kupendwa na kutuma wazo zuri vichwani mwao kwamba licha ya kupatikana na hatia ya kuwaweka mbali na jamii, bado jamii inawatambua na kuwakubali kuwa wanarekebishwa.

“Kile kitu ambacho huwa tunafanya mbali na kushabikia Chelsea, huwa tunafanya kazi ya jamii kutoa misaada ya maboma ya kuwalea watoto mayatima na maskini, na kutembelea wafungwa kama leo tumekuja katika jela la Machakos kujumuika na ndugu zetu waliofungwa."

"Chelsea Kenya tulianza mwaka 2009 na tulianza kama ukurasa wa Facebook na baada ya kujumuika mitandaoni, tuliamua kukutana kimwili na kujumuika Zaidi. Tuko na matawi Mombasa, Meru, Thika, Kitale, Kisii na pia hapa Machakos na tutaendela kwingine,” mmoja wao alisema.

Mashabiki hao walisema walichukua hatua ya kunyoosha mkono wa kutia Imani mioyoni mwa watu, ambalo ni lengo kuu la mchezo wa soka unaonuiwa kuwaleta watu pamoja katika furaha.