Staa wa Arsenal, Bukayo Saka arejea katika nchi yake ya asili, Nigeria

Mojawapo ya madhumuni ya ziara yake katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi ilikuwa ni kutoa misaada.

Muhtasari

•Huku akiwa amevalia mavazi meupe kuanzia kichwani hadi miguuni, Saka alionekana akishiriki muda mzuri na Wanigeria na kupiga picha nao.

•Miongoni mwa maeneo ambayo alitembelea nchini humo ni  kituo cha watoto yatima cha Bales of  Mercy jijini Abuja.

Image: INSTAGRAM// BUKAYO SAKA

Baada ya msimu wa EPL wa 2022/23 kukamilika, staa wa Arsenal Bukayo Saka anafurahia muda katika nchi yake ya asili ya Nigeria.

Picha na video za mshambuliaji huyo matata mwenye umri wa miaka 21 akitembea katika mitaa ya jiji la Abuja zimekuwa zikisambazwa kwenye mitandao ya kijamii. Huku akiwa amevalia mavazi meupe kuanzia kichwani hadi miguuni, Saka alionekana akishiriki muda mzuri na Wanigeria na kupiga picha nao.

Siku ya Alhamisi jioni, alichapisha video yake akiwa amendamana na waelekezi kadhaa na akatoa shukrani kwa makaribisho mazuri.

"E kuule o! Shukran kwa makaribisho mazuri," alisema kwenye Instagram.

Miongoni mwa maeneo ambayo alitembelea nchini humo ni  kituo cha watoto yatima cha Bales of  Mercy jijini Abuja.

Pia alionekana akitangamana na baadhi ya maafisa wa shirika la Msalaba Mwekundu, dokezo kwamba mojawapo ya madhumuni ya ziara yake katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi ilikuwa ni kutoa misaada.

Saka alizaliwa Ealing, London, na wazazi Wayoruba kutoka Nigeria, Adenike na Yomi Saka, na alikuwa mdogo wa watoto wawili. Wazazi wake walihamia jijini London kutoka Nigeria kama wahamiaji wa kiuchumi.

Mchezaji huyo wa timu ya taifa ya Uingereza mwenye umri wa miaka 21 ni mmoja wa wachezaji chipukizi wanaofanya vizuri kwenye Ligi Kuu ya Uingereza. Alikuwa miongoni mwa walioteuliwa kuwania tuzo ya mchezaji bora chipukizi msimu wa 2022/23 ambayo hatimaye ilipewa Erling Halaand wa Manchester City.