Raphaël Varane atilia shaka uwezekano wake kuishi hadi miaka 100 kisa kupiga mipira ya kichwa

"Mwanangu wa miaka saba anacheza mpira wa miguu, na ninamshauri asipige mpira kwa kichwa. Sijui kama nitaishi hadi 100, lakini najua kuwa nimeharibu mwili wangu ... naweza kuhisi hivyo," Varane alisema.

Muhtasari

• "Hata kama haisababishi kiwewe mara moja, tunajua kwamba kwa muda mrefu, mishtuko inayorudiwa inaweza kuwa na athari mbaya".

RAPHAEL VARANE
RAPHAEL VARANE
Image: HISANI

Beki wa Manchester United na timu ya taifa ya Ufaransa, Raphael Varane ametilia shaka uwezekano wake kuishi hadi kufikisha miaka 100.

Akizungumza na jarida la Ufaransa, L’Equip, Varane alisema kwamba amekuwa akihisi maumivu ya kichwa haswa kila mara anapopiga mipira ya vichwa, na hivyo kusema haoni akifikisha miaka 100 duniani.

Varane pia alisema kwamba amekuwa akiyaona madhara ya mipira ya vichwa kwa afya za wachezaji baadae baada ya kustaafu na hivyo amekuwa akimfunza mwanawe wa miaka 7 kutofanya udhubutu wowote wa kupiga mpira kwa kichwa.

"Mwanangu wa miaka saba anacheza mpira wa miguu, na ninamshauri asipige mpira kwa kichwa".

"Hata kama haisababishi kiwewe mara moja, tunajua kwamba kwa muda mrefu, mishtuko inayorudiwa inaweza kuwa na athari mbaya".

"Sijui kama nitaishi hadi 100, lakini najua kuwa nimeharibu mwili wangu ... naweza kuhisi hivyo," Varane alisema.

Mkongwe huyo ambaye amewahi kipiga Real Madrid alisema kwamba mapema msimu huu alihisi kutokuwa sawa baada ya kucheza mipira ya vichwa kwa Manchester United na kusema kwamba hiyo ni ishara ya kuathirika kwa afya yake ya ubongo.

"Mapema msimu huu, nilipiga mpira kwa kichwa mara kwa mara wakati wa mechi ya Man United na nilihisi uchovu usio wa kawaida katika siku zilizofuata, pamoja na kuwa na uchovu wa macho".

"Kama wanasoka wanaocheza katika kiwango cha juu, tumezoea maumivu, sisi ni kama wanajeshi, watu wagumu, ishara za nguvu za kimwili, lakini dalili hizi karibu hazionekani", aliiambia L'Équipé.