Kuokoa msimu! Leeds United yamteua kocha mpya kutoshushwa daraja

Allardyce ni kocha wa tatu kusimamia Leeds United katika msimu wa 2022/23.

Muhtasari

•Leeds United imemfuta kazi kocha mkuu Javi Garcia na mara moja kumteua Sam Allardyce kujaza nafasi hiyo.

• Makocha wawili wa awali, Garcia na Marsch walitimuliwa kufuatia msururu wa matokeop hafifu katika mechi za Ligi Kuu.

Kocha Sam Allardyce
Image: HISANI

Klabu ya Leeds United imemfuta kazi kocha mkuu Javi Garcia na mara moja kumteua Sam Allardyce kujaza nafasi hiyo.

Katika taarifa ya Jumatano, Leeds ilitangaza kuwa Garcia ataondoka pamoja na wasaidizi wake Zigor Aranalde, Mikel Antia na Juan Solla.

"Tunamshukuru Javi na timu yake kwa juhudi zao chini ya hali ngumu," klabu ilitangaza kupitia tovuti yake rasmi.

Wanne hao wametimuliwa baada ya kusimamia klabu hiyo ya Ligi Kuu ya Uingereza katika mechi kumi na mbili tu.  Walichukua usukani wa Leeds United baada ya aliyekuwa kocha, Jesse Marsch kutimuliwa.

"Mechi nne zilizosalia za msimu huu zitasimamiwa na kocha mkuu mwenye uzoefu Sam Allardyce," Leeds ilitangaza.

Sam Allardyce ambaye ana umri wa miaka 68 atalenga kuinusuru klabu hiyo isishushwe daraja kutoka Ligi Kuu. Mechi yake ya kwanza kusimamia Leeds United itakuwa dhidi ya mabingwa watetezi, Manchester City.  Baada ya hapo ataongoza klabu hiyo kucheza dhidi ya Newcastle, West Ham na Tottenham.

Allardyce ni kocha wa tatu kusimamia Leeds United katika msimu wa 2022/23. Makocha wawili wa hapo awali, Garcia na Marsch walitimuliwa kufuatia msururu wa matokeop hafifu katika mechi za Ligi Kuu.

Kwa sasa klabu hiyo imekalia nafasi ya kumi na saba kwenye jedwali la EPL huku ikiwa imecheza jumla ya mechi 34.