Patanisho: Mimi ni mwanabodaboda na mke wangu anashuku niko na mpango wa kando

“Yeye kila mara ninapomuuliza anasema niko na mpango wa kando. Mara huwa narudi kitu saa tatu hivi lakini kuna wakati mwingine naweza pata kazi ya mbali narudi 9.30 usiku…. asubuhi huwa natoka 5.30am hivi….”

Muhtasari

• Kwa upande wa mkewe Tabitha Barasa, alisema kwamba kweli anampenda mumewe lakini vitendo vyake ni vya kutiliwa shaka.

Image: RADIO JAMBO

Katika kipindi cha Gidi na Ghost kwenye redio Jambo asubuhi ya Septemba 19 kwenye kitengo cha Patanisho, Duncan Wanjala mwenye umri wa miaka 26 alitaka kupatanishwa na mke wake wa miaka 7 ambaye kila mara huvurugana.

Wanjala kutoka kaunti ya Bungoma alisema kwamba yeye hufanya kazi ya Bodaboda na hurudi nyumbani kuchelewa na kuondoka alfajiri, jambo ambalo limeleta shida katika ndoa yake ambapo mke wake ameanza kumshuku kwamba hana muda wa kukaa na yeye nyumbani na pengine ana mpango wa kando.

“Tuna watoto wawili tumekaa kwa ndoa miaka 7, huku kuvurugana kunatokea mimi nikija kuchelewa kwa sababu nafanya kazi ya bodaboda. Alipopata mtoto wa kwanza ndio mambo yakaanza kubadilika haniamini,” Wanjala alisema.

“Yeye kila mara ninapomuuliza anasema niko na mpango wa kando. Mara huwa narudi kitu saa tatu hivi lakini kuna wakati mwingine naweza pata kazi ya mbali narudi 9.30 usiku…. asubuhi huwa natoka 5.30am hivi….” Alisema Wanjala.

Kwa upande wa mkewe Tabitha Barasa, alisema kwamba kweli anampenda mumewe lakini vitendo vyake ni vya kutiliwa shaka.

Alisema kwamba huwa anatoka kwa nyumba bila kumuachia kitu na kurudi akijaribu kumuuliza huwa mkali na wakati mwingine humpiga.

“Shinda yangu kubwa mzee wangu alikuwa mzuri lakini siku hizi simuamini, anatoka 5am na hatuachii kitu na anarudi 3pm huko na mtoto wa shule kumuuliza anakuwa mkali anaanza kunipiga, akienda tena anarudi 9pm, wakati mwingine anakaa nje mpaka 11pm usiku na akikuja anaamka asubuhi anatoka bila kuacha kitu ukijaribu kumuuliza anasema nafuatilia maisha yake,” Bi Tabitha alisema.

Tabitha alisema kuna kipindi mumewe alimpiga na kumvunja mkono na akaamua kumchukulia hatua lakini akabadili mawazo alipomuona mumewe anatokwa na machozi.

“Mimi nampenda lakini kuna muda alinipiga akanivunja mkono, kurudi kwa nyumba akaona huo mkono akaanza kutoa machozi nikamhurumia sikuendelea kumchukulia hatua…” aliongeza.

Tabitha alisema mumewe hajawahi kumnunulia nguo hata moja wala watoto wake hajui huwa wanavaa aje.

Gidi alimtaka Duncan kumuomba mkewe msamaha;

“Mama Martin kusema ukweli mimi nakupenda kutoka moyoni mwangu, napenda familia yangu lakini mambo ya kunifuatilia kama nimenda kazini sitaki,” Duncan alisema huku Gidi akimkatiza.

Kwa upande wa mkewe, alisema;

“Wewe unajua vile nakupenda, hivyo vitu vyote vilivyofanyika niliacha sababu nakupenda. Mimi nakuomba uwe mwaminifu kwangu, upunguze mambo ya kunipigia kelele kama kuna kitu niulize kwa upole. Hapo mimi sina shida nitaendelea kukupenda na kukulelea watoto wako.”