"Kama Akothee ameolewa, pia wewe uolewe!" Pastor Ezekiel awaambia akina mama 'single'

Bw Ezekiel alisema alifurahi sana kumona mwimbaji huyo wa miaka 43 akiolewa.

Muhtasari

•Mchungaji Ezekiel aliitumia mfano wa Akothee kuwatia moyo akina mama single kuwa pia wao watapata wachumba.

•"Niliona nikafurahi. Nikasema ikiwa rais wa single mothers ameolewa, kina mama wote single wapate roho ya ndoa," alisema.

Denis Shweizer, Akothee, Pastor Ezekiel
Image: HISANI

Wiki iliyopita, mtumishi wa Mungu maarufu, Mchungaji Ezekiel Odero alifanya mikutano kadhaa ya maombi (krusedi) katika kaunti ya Mombasa. 

Katika siku ya kwanza ya krusedi, iliyofanyika katika mtaa wa Bombolulu, mchungaji huyo tajika alihubiri kuhusu mambo mengi ikiwa ni pamoja na mahusiano na ndoa. Pia aliwaombea waumini wenye matatizo mbalimbali ya maisha.

Bw Ezekiel aliwaombea waumini wake wa kike wasio na waume kuolewa huku akikemea nguvu za giza zinazowazuia kupata waume. Alitumia mfano wa Akothee kuwatia moyo akina mama single kuwa pia wao watapata wachumba.

"Kama ata yule binti anaitwa Akothee, aliyekuwa akiitwa rais wa kina mama single ameolewa, wewe pia uolewe kwa jina la Yesu Kristo," mchungaji huyo aliwaambia waumini waliokuwa wamejumuika kwenye mkutano huo.

Aliongeza, "Kama rais ameolewa, mawaziri, na CAS pamoja na wafanyikazi wote  wa serikali, wote waolewe."

Mtumishi huyo wa Mungu alikiri kwamba alifurahi sana kumona mwimbaji huyo wa miaka 43 akiolewa. Alisema ilimpa matumaini kwamba akina mama wengine wasio na waume watapata wenzi wa ndoa.

"Niliona nikafurahi. Nikasema ikiwa rais wa single mothers ameolewa, kina mama wote single wapate roho ya ndoa," alisema.

Mwimbaji Esther Akoth almaarufu Akothee na mchumba wake Dennis Shweizer almaarufu Mister Omosh walifunga pingu za maisha katika harusi ya kifahari iliyofanyika Windsor Golf Hotel & Country Club, Nairobi mnamo Aprili 10.

Harusi ya mama huyo wa watoto watano ilipambwa na wanafamilia, marafiki wa karibu, wasanii maarufu na wanasiasa mashuhuri nchini. Jumla ya watu wasiopungua 300 walikuwa wamealikwa kwenye hafla hiyo ya kufana.

Harusi ya Akothee na Shweizer ni yake ya pili kwani alifunga ndoa kwa mara ya kwanza na baba ya binti zake watatu, Jared Okello zaidi ya mwongo mmoja uliopita. Mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 43 hapo awali aliwahi kufichua kuwa harusi yake na Bw Jared iligharimu shilingi  2,500 pekee.