Otile Brown atoa heshima kwa shabiki wake Brian Chira, adokeza kuhudhuria mazishi yake

Msanii huyo aliomba taarifa zaidi kuhusu maandalizi ya mazishi ya Chira akidokeza kuwa anakusudia kuhudhuria.

Muhtasari

•Otile Brown ametoa heshima kwa marehemu mburudishaji wa tiktok Brian Chira aliyefariki dunia wikendi iliyopita.

•"Kwa kweli sikujua mengi juu ya jamaa huyo lakini nimekutana na video zake kama nilivyofanya hapo awali," alisema.

amemuomboleza Brian Chira
Otile Brown amemuomboleza Brian Chira
Image: INSTAGRAM

Mwimbaji maarufu wa Kenya Jacob Obunga almaarufu Otile Brown ametoa heshima kwa marehemu mburudishaji wa tiktok Brian Chira aliyefariki dunia wikendi iliyopita.

Wakati wa kipindi cha moja kwa moja kwenye mitandao ya kijamii, mwimbaji huyo mzaliwa wa pwani alizungumza kwa upendo kuhusu Brian Chira akibainisha kuwa hakufahamu mengi kumhusu.

Brown alisema mashabiki walimjulisha jinsi marehemu alivyopenda wimbo wake wa ‘One Call’, jambo lililomfanya ahisi upendo wa mwanatiktok huyo.

"Nataka kusema tu, roho yake ipumzike kwa amani. Ndo maisha hayo jamaa, leo ni yeye anaondoka, kesho ni sisi msee. Wakati mwingine unaweza ukahisi kama kifo kiko mbali nasi lakini hakiko, huwezi ukajua,” Otile Brown alisema.

Aliongeza, "Kwa kweli sikujua mengi juu ya jamaa huyo lakini nimekutana na video zake kama nilivyofanya hapo awali."

Mwimbaji huyo wa kibao ‘Dusuma’ aliendelea kuomba taarifa kuhusu maandalizi ya mazishi ya Chira akidokeza kuwa anakusudia kuhudhuria.

"Nyote mtujulishe habari kwenye blogu hizo ili tujue kuna nini. Kama ni sehemu tunaweza safari pia tuende tusapoti,” alisema.

Jumamosi alasiri, vyanzo vya habari viliripoti kwamba Chira alifariki dunia baada ya kugongwa na gari nyakati za alfajiri akitoka kuserereka klabuni.

Kwa mujibu wa ripoti ya plisi ambayo ilionwa na The Star, mwili wa Chira uliokotwa na maafisa hao majira ya asubuhi eneo la Ndenderu kaunti ya Kiambu na kusafirishwa hadi makafani ya jumla ya City.

Chira alifariki kutokana na majeraha mabaya ya kichwani.