Kila Mwanaume aliyeoa kikweli amlipe mkewe kila mwezi - Auracool

Watu walipinga suala hilo na kusema kwamba uchumi umeporomoka na hela za mambo kama hayo hazipo.

Muhtasari

• Baadhi walipinga suala hilo wakisema hiyo ni kama kuwafunga wanaume kwa nira wakati tayari mzigo mzito upo mabegani

Auracool
Image: Twitter

Mkuza maudhui maarufu kwenye mtandao wa Twitter kwa jina AuraCool ama Tweetoracle kama anavyojiita amegonga vichwa vya habari barani Afrika kwa kutoa wazo kwamba kila mwanaume mwenye ameoa basi anapaswa kumlipa mkewe kila baada ya mwezi mmoja.

Mkongwe huyo wa masoko ya kidijitali kutoka Nigeria aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter wenye wafuasi wengi akiwarai wanaume walioko kwenye ndoa wote kuwapa pozo la kila mwezi wake zao.

“Kila mwanaume wa kweli aliyeoa anapaswa kumpa mke wake posho kila mwezi,” aliandika Auracool.

Mmiliki huyo wa mtambo wa kidijitali wa habari kwa jina Auracool alizidi kufafanua zaidi ni nini anamaanisha kwa posho la kila mwezi na kusema kwamba hana maana ya hela wanaume wengi wanazoziachia wake zao kununua chakula na kuwalisha watoto nyumbani.

“Pesa ya chakula si posho,” aliweka wazi.

Katika sehemu ya maoni, paliibuka makundi mawili yaliyojibizana vikali huku wengi wa wanawake wakikubaliana mia kwa mia na ushauri huo huku wanaume wengi wakipinga vikali.

“Itakuwaje endapo katika hilo posho la kila mwezi pia hela za chakula zimo ndani kihesabu?” mmoja aliuliza.

“Vipi kwa wale wanawake walioajiriwa kazi na wanapata mshahara wa juu kuliko wanaume wao, pia wao wanafaa kuwepo katika kundi la wanawake wa kupokezwa posho?” swali lingine liliibuliwa na mtumizi mmoja wa Twitter.

Baadhi ya wanaume walisema kwamba mwanaume huyo ni ibilisi ambaye ametumwa kuvunja ndoa zilizostawi huku wakisema kwamba kama wanao huwa wanatoa tu muda wowote na si mwisho wa mwezi pekee, na kusema kwamba hiyo haifi kuhesabiwa kama posho na kumtaka aache kuvuruga ndoa za watu kwa kudanganya wanawake kwamba kuwepo katika ndoa ni kama kuajiriwa katika kiwanda ambapo mwisho wa mwezi unategemea posho na marupurupu.

Wengine walisema kwamba katika mataifa mengi ya Afrika ambapo bei za bidhaa za kawaida zimefumuka, suala kama hilo litakuwa halina maana kwa sababu zile hela kidogo wanaume wanapata zina matumizi mingi zaidi na kuongezea posho kwa mke kila mwezi ni mambo yasiyofaa.

“Katika nchi hii ambapo bei ya kila kitu ni ya juu sana, atakuwa akihangaika kuwalipia watoto karo ya shule, vyakula, mke mahitaji ya kibinafsi na kisha baadaye atawekwa pia kwenye posho ya kila mwezi? Bwana wewe tufanye tumwogope Mungu,” mmoja alilalamika.