Zari hatimaye ajibu madai ya 'kuiba' mume wa mwanadada wa Uganda

Bi Nalule alimshutumu Zari kwa 'kumuibia' mume wake Shakib .

Muhtasari

•Nalule alidai kuwa yeye ndiye mke halali wa Bw Lutaaya na hata kutoa cheti cha ndoa kuthibitisha madai yake.

•Mke huyo wa zamani wa Diamond Platnumz alijibu, "Ni watafuta kiki."

Zari Hassan, Shakib Cham, Mimi Nalule
Image: HISANI

Mwanasoshalaiti na mfanyibiashara mashuhuri  wa Uganda Zari Hassan hatimaye amejibu madai ya kuvunja ndoa ya wenyewe.

Siku chache zilizopita mwanadada mmoja wa Uganda anayeishi Marekani  alijitokeza na kumshutumu Zari kwa 'kumuibia' mume wake Shakib Cham Lutaaya.

Nalule Shamirah Sembatya almaarufu Mimi alidai kuwa yeye ndiye mke halali wa Bw Lutaaya na hata kutoa cheti cha ndoa kuthibitisha madai yake.

Zari hata hivyo ametupilia mbali madai hayo na kudai kuwa kipusa huyo anatafuta kiki tu. Mama huyo wa watoto watano alikuwa akimjibu mtumiaji wa Instagram aliyeuliza kuhusu madai ya 'kunyakua mume' wa wenyewe.

"Mkewe anasema umevunja 💔 ndoa yake, ni kweli?" @and_back_123 alihoji chini ya picha ya Zari na mpenzi ambayo alichapisha Instagram.

Mke huyo wa zamani wa Diamond Platnumz alijibu, "Ni watafuta kiki."

Kulingana na cheti ambacho Nalule alionyesha,yeye na Shakib walifunga ndoa mwezi Juni 2016 baada ya kuchumbiana kwa muda.

Nalule pia alidai kwamba mnamo Mei 2017 alimpa Shakib visa ya Amerika kama mchumba wake, hivyo kumpa uwezo wa manufaa kadhaa.

Kipusa huyo sasa alimshtumu mpenziwe Zari kwa kuikimbia ndoa iliyofungwa kisheria ili kuwa na Zari ambaye ni maarufu na tajiri zaidi.

Hivi majuzi Zari alifichua kuwa tayari amepiga hatua ya kukutana na wazazi wa mpenzi wake Shakib Lutaaya na kubainisha kuwa yuko tayari kupeleka mahusiano yao ya miezi kadhaa katika kiwango cha juu zaidi.

"Shakib alinipeleka kuwaona wazazi wake na ilikuwa nzuri sana," Zari alisema.

Mahusiano ya Zari Hassan na Shakib yamekuwa yakikosolewa sana hasa kwenye mitandao ya kijamii suala kuu likiwa tofuati zao za umri. Zari ana umri wa miaka 42 ilhali mpenziwe alitimiza miaka 31 hivi majuzi.

Mama huyo wa watoto watano hata hivyo alibainisha kuwa wazazi wa Shakib hawakuashiria tatizo lolote na mahusiano yao na kubainisha kuwa mkutano wao ulikuwa mzuri.

“Alinipeleka kuonana na wazazi wake na walikuwa wazuri sana, na sikumbuki hata kidogo wakilalamika kuhusu uhusiano huo,” mzaliwa huyo wa Uganda alisema na kuongeza kuwa hatajitetea kabisa.

Zari pia alifichua kuwa anapanga kuongeza watoto zaidi na Shakib lakini akabainisha kuwa si kwa sababu ya shinikizo la umma.