Manzi wa Kibera aweka wazi uhusiano wake halisi na marehemu Mzee Nzuki baada ya mazishi

Mwanasoshalaiti huyo kutoka Kibera hakuhudhuria maziko ya Mzee Nzuki yaliyofanyika Jumatano, Mei 1.

Muhtasari

•Mrembo huyo kutoka Kibera aliweka wazi hakuwahi kuwa na uhusiano wowote wa kimapenzi na marehemu Mzee Ndunda.

•Ni watu wachache tu waliohudhuria hafla ya maziko ya mzee huyo mwenye umri wa miaka 67 kwenye makaburi ya Langata.

Manzi wa Kibera na marehemu Mzee Nzuki
Image: INSTAGRAM// MANZI WA KIBERA

Mwanasosholaiti wa Kenya aliyezingirwa na utata mwingi Sharon Wambui almaarufu Manzi wa Kibera hatimaye ameweka wazi ukweli  kuhusu uhusiano wake halisi na marehemu Mzee Sammy Ndunda Nzuki ambaye aliaga dunia hivi majuzi.

Katika chapisho la Instagram siku ya Alhamisi asubuhi, mrembo huyo kutoka Kibera aliweka wazi kuwa hakuwahi kuwa na uhusiano wowote wa kimapenzi na marehemu Mzee Ndunda.

Alibainisha kwamba alifanya vipindi tu na mwanamume huyo wa miaka 67 kwa ajili ya kiki za mtandaoni.

“Sikuwa natoka kimapenzi na Marehemu Mzee Nzuki. Yalikuwa maudhui ya mtandaoni. Si ya kweli,” Manzi wa Kibera alisema Alhamisi asubuhi.

Alifichua hayo baada ya blogu moja ya hapa nchini kumtaja Mzee Nzuki kama mpenzi wake wakati ikiripoti kuhusu mazishi yake siku ya Jumatano.

Manzi wa Kibera hakuhudhuria maziko ya Mzee Nzuki yaliyofanyika Jumatano, Mei 1.

 Katika video iliyovuja mtandaoni, ni watu wachache tu waliohudhuria hafla ya maziko ya mzee huyo mwenye umri wa miaka 67 kwenye makaburi ya Langata.

Sammy Ndunda Nzuki alifanyiwa hafla rahisi ya maziko.

Chali wa Kibera aliibuka na kufichua kuwa Manzi wa Kibera almaarufu Wambo hakuwa sehemu ya maziko hayo. Yeye ni meneja wake.

"Nataka tu kuwajulisha kuwa Mzee Nzuki alizikwa leo Langata na hakukuwa na vyombo vya habari kwa sababu familia haikutaka uwepo wa media, walikua tu kutaka kumpatia mzee mazishi yenye heshima isiyo na kamera," Chali wa Kibera alieleza.

Aliongeza, “Ingawa nina video na picha chache lakini naomba niwafahamishe kuwa mzee amezikwa leo huko Langata na familia yake na mimi au Manzi wa Kibera hakuna aliyealikwa na ninaelewa kabisa maana labda walidhani tukienda tunaeza enda na. watu wa media."

Chali wa Kibera alishiriki maelezo ya hatua yao inayofuata akisema, "Labda tutapata muda wetu wa kwenda kuangalia kaburi ambayo walisema ni sawa,"