"Vibabu sio hobby ama kazi!" Zari Hassan amshambulia mwanablogu kwa kumfanya kuwa mada

Muhtasari

•Mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz amemshtumu Kimambi kwa kumfanya mada kuu ya mazungumzo kwenye App yake.

•Zari amesisitiza kwamba yeye ni tajiri anayeweza kumudu maisha ya kifahari na kununua vitu vya thamani kubwa.

Image: INSTAGRAM// ZARI HASSAN

Mwanasoshalaiti na mfanyibiashara mashuhuri Zari Hassan ameendelea kumkashifu mwanablogu Mange Kimambi kwa kile anachokiita kuingilia maisha yake.

Mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz amemshtumu Kimambi kwa kumfanya mada kuu ya mazungumzo kwenye App yake.

Zari amesema kwamba mwanablogu huyo wa Tanzania amekuwa akijinufaisha kwa kumchafulia jina na kueneza uvumi hasi kumhusu. Amedai kwamba Kimambi angekuwa hohe hahe iwapo angesita kumzungumzia.

"Tutumie akili kidogo. Vibabu sio hobby ama career. Atafute kazi, mimi hapa namnunulia chakula, tena anishukuru sana. Bila Zari, App haitembei. Nampa siku mbili ajiweke, aongelee maisha yake na vibabu vyake uone kama atakuwa na traffic. Zari ndo mpango. Bila Zari hawezi lipa bills, vibabu vyeupe tu lakini havina pesa. Kashamba rangi ndo inakadanganya" Zari alimpasha Kimambi.

Mama huyo wa watoto watano amekerwa na kitendo cha Kimambi kukosoa utajiri wake na mtindo wake wa maisha.

Zari amesisitiza kwamba yeye ni tajiri anayeweza kumudu maisha ya kifahari na kununua vitu vya thamani kubwa.

"Nanunua manyumba, magari, apartment za watoto wangu, naenda na 1st class Emirates. Leo niambie siwezi kununua begi za dola 2000-4000" Amesema.

Zari pia amewakosoa wafuasi wa  mwanablogu huyo kwa kukubali maneno hasi anayoeneza. Amedai kwamba Kimambi amekuwa akiishi maisha ya kitajiri bandia ilhali yeye ni fukara.