Masanja: Simwachi mke wangu hata kama nitamfumania akila uroda na mwanaume

Sisi tumeoana mpaka kitutenganishe kifo - Masanja Mkandamizaji.

Muhtasari

• Masanja alisema hata ndoa zote ziishe leo na kesho waambiwe waoe upya basi atamrukia mke wake yule yule.

• Alikuwa akiyazungumza haya baada ya skendo ya kujiua kwa katibu wa kanisa lake kuhusishwa na kutoka kimapenzi na mkewe.

Mchungaji Masanja Mkandamizaji na mkewe
Mchungaji Masanja Mkandamizaji na mkewe
Image: Instagram

Mchekeshaji aliyegeukia uchungaji Masanja Mkandamizaji kwa mara ya kwanza tangu kutua nchini Tanzania akitokea Marekani, amezungumzia suala linalozidi kutokota kuhusu sababu za kujitoa uhai kwa katibu wa kanisa lake.

Wiki jana pamoja pia na wiki huu skendo ya kujiua kwa katibu wa kanisa la Masanja Mkandamizaji liitwalo Feel Free imekuwa ikihusishwa kwamba alikuwa anatoka kimapenzi na mke wa baba mchungaji ambaye ni Mkandamizaji.

Masanja akizungumza na waumini wake katika video ambayo imesambazwa mitandaoni amewahakikishia kwamba yeye hayuko tayari kumwaacha mkewe leo, kesho wala akhera, liwake jua, inye mvua!

Mchungaji huyo alitokea mfano kuwa hata kama ndoa zote zilikuwa zinaisha leo hii halafu tena kesho Mungu akatoa kibali cha watu kufanya ndoa upya basi yeye atamrukia mke wake huyo huyo ambaye anazungulukwa na skendo ya kutoka kimapenzi na katibu aliyejiuwa kutokana na kile kilisemekana kuwa wivu wa kimapenzi.

Aidha wengine waling’aka kuwa katibu huyo alijiua kwa kukataliwa kimapenzi na mke wa mchungaji, na hata kuacha barua ndefu akijitoa kwa hali na mali jinsi alivyokuwa anampenda Monica, mke wa mchungaji Masanja Mkandamizaji.

Katika tamko ambalo sasa limekuwa gumzo, Masanja Mkandamizaji aliwaambia waumini wa kanisa lake kuwa hata ikatokea amemfumania mkewe moja kwa moja na mwanaume mwingine wakishiriki mapenzi, hawezi kumpiga hata kidogo bali atamshika mkono na kumutizama jamaa yule, akiona hatommudu kwa nguvu basi atamshika mkewe na kuondoka naye.

“Kwa mfano mimi sio mchungaji wala hakuna kanisa linahusika, na nimemkuta huyu dada akiwa kama mke wangu, moja kwa moja anakula uroda na jamaa. Namkamata kwanza mke wangu kwa mkono halafu nampima yule jamaa; nammudu au simmudu. Nikiona hii ngoma siiwezi kuimudu atanipasua, ninaondoka na mke wangu. Sisi tumeoana mpaka kitutenganishe kifo,” mchungaji Masanja Mkandamizaji alisema huku umati wa waumini ukipasuka kwa vicheko.