Pritty Vishy: Kama unataka kutoa hii mali sokoni lazima uwe na pesa

"Nyie muanze kuingia DM yangu usaili unaendelea kwa dm yangu hakikisha uko na pesa" - Pritty Vishy.

Muhtasari

• Mwanablogu huyo alisema anatafuta mwanamume wa kujivinjari naye siku ya wapendanao ambayo ni Februari 14.

Vishy atangaza kutafuta mume
Vishy atangaza kutafuta mume
Image: Instagram

Mwanablogu Pritty Vishy ametangaza kuwa anatazamia kupata mwanamume mzuri mwenye pesa huku siku ya wapendanao ya Valentino ikikaribia.

Vishy ambaye amekuwa singo tangu mwaka jana walipoachana na msanii Stevo Simple Boy alidokeza kuwa kwa sasa anatafuta mwanaume wa kutoka naye siku ya wapendanao, huku akitaja vigezo muhimu vya mwanamume huyo.

“Swali ni hakuna mwanamume wa maana hapa nje mwenye anaona huu mzigo? Haki siku ya wapendanao ya Valentino inakaribia naomba mniondoe sehemu hii ya upweke,” Vishy alisema kwenye picha nzuri ambazo alizipakia Instagram yake.

Aliendelea kutoa muongozo zaidi akisema mwanamume yeyote mwenye anaona ana uwezo wa kuhimili na kumudu mahitaji yake basi asisite bali akimbie moja kwa moja kwenye DM yake ili amfanyie tathmini kama anatosha mboga au la.

Alitoa tahadhari kuwa hatokubali mwanamume yeyote mwenye hana hela. Yoyote mwenye anafaa kumfuata faraghani anafaa kwanza kuhakikisha kuwa mfuko wake ni mzito.

“Nyie muanze kuingia DM yangu usaili unaendelea kwa dm yangu🤣🤣hakikisha uko na pesa rafiki yangu sababu hicho ndicho kigezo cha kwanza. Ninamaanisha na sitaki mzaha,” Pritty Vishy alisema.

Vishy na Stevo waliachana mwaka jana mwanzoni, huku wakikandiana vikali na kuchafuana kwa maneno ya nguoni kila mmoja akijaribu kujionesha kuwa ni msafi na mkosewa.

Mwanablogu huyo chipukizi amekuwa akijitahidi sana tangu kipindi hicho, huku kwa wakati mwingine akitumia sekeseke za kuachana kwake na Stevo kuteleza nazo kwa faida yake.

Hivi majuzi amedhibithishwa kwenye mtandao wa Instagram na wabaya wake waliona siku mrefu kwani alijishaua na kujikosha mithili ya tausi.