Diamond afichua sababu ya kukosekana kwa wasanii wa kike Wasafi kando na Zuchu

Zuchu ndiye msanii wa pekee wa kike hadi sasa kusainiwa kwenye lebo ya Wasafi lakini pia ndiye amekuwa akiwakilisha jinsi ya kike katika tamasha la Wasafi.

Muhtasari

• Diamond alijibu kwa njia ya kuashiria kwamba huenda walijaribu kuwafikia wasanii wa kike lakini juhudi zao zilibuma kwa kuvimbiwa na wasanii hao.

• Hata hivyo, pia alisema kwamba wasanii wanaohisi kufungiwa nje wasife moyo kwani bado tamasha hilo linaendelea na huu ndio mwanzo tu.

Diamond Platnumz
Diamond Platnumz
Image: Screengrab

Msanii na mkurugenzi mtendaji wa Wasafi Diamond Platnumz amejibu swali ambalo limekuwa likiulizwa kwa muda mrefu kuhusu kutokuwepo kwa wasanii wa kike katika lebo na tamasha linaloendelea la Wasafi.

Diamond alikuwa akifanya mkutano na vyombo vya habari kupromoti chapa ya Pepsi ambayo imekuwa mstari wa mbele kufadhili tamasha hilo ambalo limekuwa likifanyika katika mikoa mbalimbali tangu mwezi jana.

Aliulizwa mbona katika tamasha hilo kumekuwa na wasanii mbalimbali tena wengi wakiwa ni wa kiume huku kwa upande wa wasanii wa kike, bendera yao imekuwa ikipeperushwa na Zuchu pekee hali ya kuwa Bongo kuna makumi ya wasanii wa kike wanaofanya vizuri na pia walio na fanbase tiifu kwao.

Diamond alijibu kwa njia ya kuashiria kwamba huenda walijaribu kuwafikia wasanii wa kike lakini juhudi zao zilibuma kwa kuvimbiwa na wasanii hao.

“Lakini unajua wakati mwingine wasanii wanaweza kuwa wako na ratiba zao kwa hiyo inakuwa vigumu kuwapata kwa wakati tunaowahitaji. Lakini tulijitahidi kuwaingiza wasanii mbalimbali. Lakini pia wasanii tuliwapigia simu waje katika tamasha wanatuletea mapozi... wasituletee pozi, ukileta pozi mimi nakukata. Unaelewa? Kwa sababu hata usipokuwepo shoo itajaa tu!” Diamond alisema kwa tambo.

Pia aliwashauri wasanii kujaribu kuwa waelewa ili wote wapate nafasi ya kushiriki katika tamasha hilo la kila mwaka.

“Wasanii tukuwe na flexibility ili wote tushiriki kwa sababu sisi tunatamani tuwaite wasanii tofauti sana sana.”

Msanii huyo pia alisema ni kigezo kipi wanachokiangalia ili kuwaalika wasanii mbali mbali kwenye tamasha hilo.

“Ukiangalia, wasanii wanaenda waki-rotate lakini kiuhalisia ni ngumu sana kuwaacha wasanii ambao wamefanya vizuri katika tamasha la awali na kuwachukua wengine tu kisa unataka kuonesha umebadilisha. Sisi tulitangaza kabla kwamba tunakuja katika Wasafi Festval na kumtaka kila msanii kuweka mawe…tuliwaambia wasanii kwamba ngoma zao zitapigwa kwenye rotation na wale watakaokuwepo kwenye peak wataingia kwenye Wasafi Festival,” alisema.

Hata hivyo, pia alisema kwamba wasanii wanaohisi kufungiwa nje wasife moyo kwani bado tamasha hilo linaendelea na huu ndio mwanzo tu.

“Sasa mimi niwaambie kwamba Wasafi Festival bado inaendelea, ndio mwanzo tuko mikoa minne, bado mikoa Zaidi ya kumi. Watu waendelee kutoa nyimbo zao, waendelee kufanya vitu. Wanaendelea kuingia tofuati tofauti, ukiangalia sasa hivi wanaotumbuiza ni tofauti tofauti,” alisema akisisitiza kwamba Wasafi Festival si tamasha la Wasafi tu bali ni tamasha la kitaifa.