Mgonjwa (Diamond) na daktari wake (Zuchu) waamsha popo stejini Wasafi Festival

“Unanipenda mimi, unanitaka pia, unaniaminia, umeniridhia?” waliulizana kwa kutumia baadhi ya mishororo kwenye collabo yao ya Mtasubiri.

Muhtasari

• Akiwa kama tabibu wa monjwa [Diamond], Zuchu alimkaribia na kuanza kumpapasa jukwaani huku mashabiki wao wakishindwa kuzuia vaibu zito.

Diaond na Zuchu kwenye ubora wao jukwaani.
Diaond na Zuchu kwenye ubora wao jukwaani.
Image: Screengrab//WasafiMedia

Diamond ambaye awali alikuwa amefichua kwamba alikuwa amelazwa kabla ya shoo yake ya Arusha kwenye tamasha la Wasafi Festival alifanya kufuru jukwaani akiwa na anayesemekana kuwa mpenzi wake Zuchu.

Wawili hao ambao wamekuwa wakiendeleza ngonjera kuwa ni wapenzi tangia mapema mwaka jana safari hii walitumbuiza pamoja kwenye ukumbi na maudhui yao yalikuwa igizo la mgonjwa na daktari wake.

Diamond baada ya kupakia picha na video kwenye instastories na pia kuandika aya ndefu kuhusu kuugua ghafla, akiibukia kwenye ukumbi huo akiwa na mavazi kama mgonjwa.

Kwa upande mwingine Zuchu alitokea akiwa na joho la kitabibu, kichwani kilemba chenye ishara nyekundu ya alama ya kujumulisha kuashiria mazingira mazima ya hospitalini.

Akiwa kama tabibu wa monjwa [Diamond], Zuchu alimkaribia na kuanza kumpapasa jukwaani huku mashabiki wao wakishindwa kuzuia vaibu zito.

Wawili hao waliimba baadhi ya nyimbo zao za pamoja huku Zuchu akimgusagusa Diamond kwenye kifua na paji la uso kama afanyavyo nesi kutumia kiganja chake kupima hali ya joto ya mwili wa binadamu.

“Unanipenda mimi, unanitaka pia, unaniaminia, umeniridhia?” waliulizana kwa kutumia baadhi ya mishororo kwenye collabo yao ya Mtasubiri.

Wawili hao walitumia wimbo huo kutema tambo kwa wanaoonea gere penzi lao wakiwataarifu kwamba watasubiri sana kwani penzi lao haliko karibu na kupatwa na nyufa zozote.

Hii inakuja siku chache baada ya walimwengu kueneza uvumi kwamba Diamond amemuacha Zuchu na kurudi kwa mama mtoto wake kutoka Kenya Tanasha Donna ambaye walionekana naye kwa kipindi cha siku kadhaa wakati wa kusherehea siku yake ya kuzaliwa inayofungamana na ile ya mtoto wake Naseeb Junior.

Zuchu kwa kuwajibu, alikariri maneno hayo akisema kwamba wengi wanaosubiri jambo dogo litokee ili kupata nafasi ya kuzungumzia kuachana kwao ni wale ambao wamejawa na husda kwamba ni vipi ameweza kumudu kwenye penzi na Diamond kwa muda mrefu hali ya kuwa msanii huyo ameshindikana kwa vidosho wengine.