Kanye West kutumbuiza katika uwanja wa Nyayo Desemba mwaka huu

Kanye amekuwa akigonga vichwa vya habari kwa mfululizo wa miaka miwili iliyopita tangu ndoa yake na mwanamitindo Kim Kardashian ilipovunjika baada ya takribani miaka 12.

Muhtasari

• Ye, kama anavyojiita mjasiriamali huyo wa Yeezy alifichua kwamba atazuru mataifa 3 ya Afrika yakiwemo Misri, Nigeria na Kenya.

Kanye West
Kanye West
Image: BBC NEWS

Wapenzi wa muziki wa HipHop nchini Kenya wana kila sababu ya kutabasamu kwa mwaka 2024 kwani msanii mkali wa rap kutoka Marekani, Kanye West ametangaza kuwa atazuru nchini Kenya na hata kutumbuiza katika uwanja wa kitaifa wa Nyayo mwishoni mwa mwaka.

West kupitia kwa mtandao wake wa Instagram alichapisha kuwa hajawahi ruhusiwa kufanya matamasha kwa muda sasa na mwaka huu amepata nafasi ya kipekee kurejelea matamasha yake huku akisema mwaka huu atakuwa na ziara ya kipekee katika bara la Afrika.

Ye, kama anavyojiita mjasiriamali huyo wa Yeezy alifichua kwamba atazuru mataifa 3 ya Afrika yakiwemo Misri, Nigeria na Kenya.

Nchini Misri, atatumbuiza kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Cairo, na huko Nigeria, mashabiki wake watakutana naye katika Jiji la Eko Energy.

Kanye pia amepangwa kuzuru sehemu zingine za ulimwengu, miongoni mwao Uhispania, Argentina, Uingereza, Australia, Japan na Mexico katika ratiba iliyojaa ya mwaka mzima.

Maelezo ya safari yake aliyopanga kwenda Kenya hayajawekwa wazi, lakini hili ni jambo ambalo mashabiki wa rap nchini wanatazamia.

Muziki wa hip-hop wa Marekani hufurahia ushabiki mkubwa nchini Kenya, nchi ambayo pia imetoa wanamuziki wake wa kufoka. Ni pamoja na Khaligraph Jones, Octopizzo miongoni mwa wengine.

Kanye amekuwa akigonga vichwa vya habari kwa mfululizo wa miaka miwili iliyopita tangu ndoa yake na mwanamitindo Kim Kardashian ilipovunjika baada ya takribani miaka 12.

Msanii huyo ambaye si mzungumzaji sana alikwenda mbele na kumuoa mfanyikazi wa ubunifu katika kampuni yake ya Yeezy, Bianca Censori na ambaye wamekuwa wakitembea na yeye katika kila sehemu.

Hata hivyo, Kanye amekuwa akipata shtuma nyingi watu wakidai kwamba anamtumia mrembo huyo wa Australia kama roboti ambapo haruhusiwi kusema chochote kwa waaandishi wa habari pindi wanapomfumania mitaani.