EXCLUSIVE

Meneja wa Stevo Simple Boy ataja chanzo cha stress kwa msanii wake

Meneja alifichua kwamba ni kweli katika kipindi cha kama siku nne hivi hawajakuwa katika maelewano mazuri na msanii huyo.

Muhtasari

• Mstado ambaye pia ni msanii alieleza kinagaubaga kwamba chanzo cha kuvunjika kwa uhusiano mwema na msanii wake ni kutojisimamia.

Stevo Simple Boy na meneja wake Chingiboy Mstado
Stevo Simple Boy na meneja wake Chingiboy Mstado
Image: WhatsApp//Chingiboy Mstado

Siku moja baada ya msanii Stevo Simple kuzua moja ya tukio la kushtuza baada ya kuzirai akiwa anatumbuiza jukwaani kwenye kipindi kimoja cha runinga, meneja wake amefunguka kwa undani kinachoendelea katika maisha ya faraghani ya msanii wake.

Stevo Simple Boy baada ya kuanguka jukwaani, baadae alidokeza kupitia ukurasa wake Instagram kwamba anapitia msongo wa mawazo na kumtaka meneja wake kurudi ili wasukume kazi pamoja.

Katika mazungumzo ya kina na Moses Sagwe wa Radio Jambo, meneja wa Stevo Simple Boy, Chingiboy Mstado alifichua kwamba ni kweli katika kipindi cha kama siku nne hivi hawajakuwa katika maelewano mazuri na msanii huyo.

Mstado ambaye pia ni msanii alieleza kinagaubaga kwamba chanzo cha kuvunjika kwa uhusiano mwema na msanii wake.

Meneja huyo ambaye alimshika mkono Stevo baada ya kutengwa alizungumzia pia kuzirai kwa msanii wake jukwaani, na kusema kwamba ni kweli huenda ako na msongo wa mawazo lakini pia ni kutokana na kutumia nguvu nyingi jukwaani.

“Nafikiri [kuzirai] ni kwa sababu alitumia nguvu nyingi pale kwa steji, ndio maana alikuwa na stress nyingi hivyo. Hatujakuwa katika maelewano mazuri kuhusu tu ya hayo mambo ambayo yanaendelea kwa mitandao. Stevo mwenyewe hawezi jiongelelea, ni sawa tunaelewa ni mpole lakini anafaa asimame ajiongelele, ajue hili ni sawa na hili si sawa,” Mstado aliongeza.

Hata hivyo, Mstado aliweka wazi kwamba hajavunja mkataba na Stevo bali alijipa likizo fupi mbali na msanii huyo ili yeye [Stevo] apate kujifunza na kuthamini mchango wake katika safari yake ya kimuziki.