Pigo kwa Chef Maliha, Guinness WR ikitupilia mbali rekodi yake kupika kwa saa 90 mfululizo

“Kwa ushauri wa meneja wangu, sina budi kukujulisha kuwa niliondolewa kwa kosa 1 lililofanywa wakati wa mapumziko yangu. Siko sawa kwa sasa. Ninaomba msamaha wako kwa kuwakatisha tamaa wote. Haikuwa rahisi"

Muhtasari

• Maliha kupitia ukurasa wake wa Instagram alitoa taarifa mbaya kwa mashabiki wake akisema kwamba rekodi hiyo aliyojaribu kuiweka haikufaulu kusimama.

Mpishi mkenya Maliha Mohammed
Mpishi mkenya Maliha Mohammed
Image: INSTAGRAM

Mpishi Maliha Mohammed kutoka Mombasa Kenya hatimaye amevunja kimya chake kuhusu hali ya rekodi yake ya kupika kwa saa 90 mfululizo ambayo alijaribu kuifanya mwishoni mwa mwaka jana.

Maliha kupitia ukurasa wake wa Instagram alitoa taarifa mbaya kwa mashabiki wake akisema kwamba rekodi hiyo aliyojaribu kuiweka haikufaulu kusimama.

Mpishi huyo ambaye kipindi cha kupika alizingirwa na watu maarufu mbalimbali ambao walijiunga na yeye kumpa motisha ya kuweka rekodi hiyo, alisema kwamba Guinness World Records walikataa kuisindika rekodi hiyo wakitaja kuwepo kwa makosa wakati wa mfululizo huo wa kupika.

Maliha hata hivyo aliwaomba radhi mashabiki wake lakini pia wafadhili wake kwa kuwaangusha kwani rekodi hiyo ambayo alikuwa anatarajia ingethibitishwa na kuwekwa kwenye vitabu vya rekodi vya Guiness imekunywa maji hivyo.

“Habari, Assalamun aleykum. Inasikitisha sana kuwajulisha familia yangu, marafiki, mashabiki, wafadhili, wafuasi, na kila mtu ambaye alionyesha upendo na kuniunga mkono ️ kuelekea safari yangu ya Novemba ya mbio za marathoni.”

“Kwa ushauri wa meneja wangu, sina budi kukujulisha kuwa niliondolewa kwa kosa 1 lililofanywa wakati wa mapumziko yangu. Siko sawa kwa sasa. Ninaomba msamaha wako kwa kuwakatisha tamaa wote. Haikuwa rahisi 😕 😪 😔 ila najua mungu ana mipango mingine na mimi in shaa Allah maana kilichokusudiwa utakipata kwa urahisi. Kwa wale waliokuwa wakisubiri rekodi hii, 😭😭😭 samahani sana 😞” Maliha alithibitisha.

Mwaka jana baada ya kuweka rekodi hiyo na kushuhudia kimya kutoka kwa GWR, Chef Maliha katika mazungumzo na Moses Sagwe wa Radio Jambo alisema kwamba alikuwa anasubiria majibu huku pia akiwa na matumaini ya kutuzwa na rais wa nchi, William Ruto.

Kwa mujibu wa Maliha, rais Ruto wakati anatunuku mwanariadha Faith Kipyegon kwa kuweka rekodi mpya kwenye riadha, alisema kuwa Mkenya yeyote atakayeweka au kuvunja rekodi atatuzwa.

“Ninategema zawadi kutoka kwa rais wetu. Natarajia atanipa msaada wa kifedha. Bado hajatoa maoni yoyote lakini naamini ashafikishiwa ujumbe kupitia mitandao ya kijamii. Alisema ahadi yake kwamba anayevunja rekodi yoyote ya dunia atapewa zawadi na serikali,” Maliha alisema.