Naibu wa Rais William Ruto ni mwanasiasa ambaye kuanzia mwanzo alifahamu anataka nini baada ya muda gani . mkakati wake huenda unafaulu kwa sababu aeweza kuteka ndimi za wengi ni mojawpao ya watu ambao wameangaziwa na vyombo vya habari kuanzia wakati waliposhinda uchaguzi pamoja na rais Uhuru Kenyatta mwaka wa 2013 . Ruto mwanzoni alipiga shughuli zake kimyakimya wakati wa hatamu ya kwanza ya serikaoli ya Jubilee .Mbinu yake mwanzoni ilikuwa kuwashawishi viongozi wengi iwezekanavyo kuingia katika kambi yake na kuunga mkono ari yake ya kutaka kumrithi rais Uhuru kenyatta mwaka wa 2022 . Uchu wake kutaka uongozi huenda pia umechangia kuvuruga uhusiano wake na rais Kenyatta kwa sababu wadadisi wanahisi azma yake imepepezea chini jitihada za Kenyatta kuacha urithi mzuri kwa taifa .Hakuna ambacho kimemzuia Ruto kuendelea na kampeini zake za chini wa chini kuchukua uongozi na weledi wake kujieleza ,ukakakamavu na mtindo wake wa siasa utafanya kuwa vigumu kumpuuza kama mgombeaji wa urais mwaka wa 2022. Kando na ngome yake ya Rift valley kuwa kapuni tayari ,Ruto amefaulu kufanya jambo ambalo wanasiasa wengi wangeshindwa kulifanya –kuwashawishi takriban nusu ya viongozi kutoka eneo la rais ,Mlima Kenya kuwa nyuma yake . Endapo yanayosemwa ni kweli kwamba rais Kenyatta amebadilisha nia kuhusu kumwunga mkono Ruto mwaka wa 2022 , mbinu ya Ruto imebainika wazi itakuwa ni kuwaendea wakaazi wa mlima Kenya moja kwa moja na sio kutegemea mawakala wa ‘katikati’ kuzungumza kwa niaba yake .Ari ya Ruto kutaka kumrithi mkuu wake Kenyatta ,imezua mgawanyiko katika chama cha Jubilee na pia mpasuko wa kimaoni kati ya watu wa jamii ya kikuyu . Migawanyiko kama hiyo haiwezi kusababishwa na mwanasiasa ambaye hajajenga ushawishi wa kutosha kuweza kushinda urais . Endapo hapatatokea muungano thabiti wa wa kipekee wenye viongozi wenye uwezo wa kumkabili Ruto vilivyo,huenda basi Naibu wa rais akawa rais wa 5 Wa Jamhuri ya Kenya .
2.Raila Odinga .
Tinga kama anavyojulikana na watani zake ,inaripotiwa hajazima ari ya kutaka kuliongoza taifa .Mwafaka kati yake na rais Kenyatta uliozaa BBI umezua mhemko kwamba huenda ni njama ya kumsaidia kuingia ikulu . Raila ana historia ndefu ya kupigania mageuzi nchini Kenya na pia mfumo wa siasa za vyama vingi . Lakini baada ya utata uliozingira chaguzi kuu za kuanzia mwaka wa 2007,2013 na 2017 wengi wa wafuasi wake walianza kupoteza matumaini kabisa kuhusu uwezo wake kutoa ushindani unaohitajika tena kunyakua ushindi katika uchaguzi wa urais .Maajuzi Odinga ametimu umri wa miaka 75 na endap atawania urais mwaka wa 2022 ,atakuwa dite mgombeaji mkongwe sana .Hilo huenda litakuwa Baraka kwake ama laana .Huenda akajitangaza kama mtu mwenye uzoefu na busara yake inahitajika uongozini kwa sababu ya umri lakini wapinzani wake watamtaja kama ‘mzee’ ambaye hatokuwa na nguvu za kuliongoza taifa kwa maono mapya na ya kisasa . Inangojewa na wnegi kuona iwapo azma yake kuwania kiti hicho itaungwa mkono na rais Uhuru Kenyatta hasa baada ya ushirikiano wao wa karibu katika muhula huu wa pili na wa mwisho wa Kenyatta .Odinga yungali hawezi kupuuzwa kwa sababu ya uwezo wake kuwavutia wananchi lakini ngome yake ya magharibi imevamiwa na naibu wa rais William Ruto na huenda asiweze kudhihirisha ushawishoi mkubwa kama hapo awali bila kupiga kibarua cha ziada . Takriban wanasiasa wote wakuu nchini ,wameweza kuzipata nafasi zao kwa ajili ya kuhusishwa na odinga au kumpinga kinara huyo wa ODM .Je,ataweza kupata msisimko wa kumrejesha tena kileleni mwa kampeini za kuweza kushinda urais?
3.Musalia Mudavadi .
Musalia Mudavadi ni mwanasiasa ambaye wengi wanahisi ni mtu mzuri na aina ya wanasiasa ambao hutajwa kama ‘wangwana’. Mafanikio ya Mudavadi hata hivyo yatategemea vitu mbali mbali kwa sababu kinbinafsi ,hajaweza kujenga mtandao wa uungwaji mkono kama Ruto na Odinga .Licha ya kuwa katika serikali na kushikilia nyadhfa kuu uongozini ,Mudavadi amesalia kama jina lake ‘Musalia’-hajajitokeza na makali ya uchu wa kutaka uongozi lakini amesalia kuwepo katika fikra za wakenya wanaomzingatia kama anayweza kuwa rais mzuri . Kwanza ,Mudavadi ataweza kuwa rais endapo ngome yake ya magharibi mwa Kenya itaungana ili kumpiga jeki . Ushawishi na muungano wa jamii ya waluhya ni jambo ambalo litamfanya Mudavadi kutochukuliwa kwa mzaha kwa sababu kura za eneo hilo zinaweza kuamua ni nani atakayekuwa rais wa tano .Pili ,kuna viongozi wanaohisi kwamba Mudavadi ndiye kiongozi wa hadhi ya juu ambaye hazui mgawnayiko mkubwa miongoni mwa wakenya .kwa hivyo anaweza kutumia kama Rais wa ‘Kuliunganisha’ taifa kwa ajili siasa zake haziligawanyi taifa katikati kama vile siasa za naibu wa rais Ruto na kiongozi wa ODM Raila odinga .endapo atafaulu kuwashawishi nusu ya vigogo walio katika mrengo wa Ruto,na nusu ya vigogo katika mrengo wa Raila pamoja na usaidizi wa mtandao wa zamani wa chama cha KANU,Musalia Mudavadi anaweza kuwa rais wa tano wa Jamhuri ila hayo mawili hayatoshi kwa sababu siasa hubadilika kila sekunde na matukio yasioweza kutabirika yanaweza kubadilisha kabisa mkondo wa mambo .
4.Kalonzo Musyoka
Makamu wa zamani wa Rais Kalonzo Musyoka ,hangedhaniwa angelikuw akatika hali hii ya kupigania urais kwa sababu wakati mmoja nyota yake ilikuwa imepaa juu zaidi lakini siasa zina mabo kweli .Musyoka ,inaripotiwa kwa wakati mmoja aliokuwa makamu wa rais katika utawala wa rais Mwai Kibaki alikuwa na uhakika kwa kumrithi Kibaki . Alikuwa muamonifu kwa Kibaki na kundi lake na alifahamu fika kwamba wakati wa uchaguzi ,angeweza kuungwa mkono na rais mstaafu .Ila ilipofika wakati wa uchaguzi ,mambo yalibadilika na hakuweza kupita ‘katikati’.Kalonzo ameweza kujikanganya kuhusu iwapo anataka kuwa rais au kuwasaidia viongozi wengine kuchukua kiti hicho.Ukosefu wake wa kuchukua msimamo thabiti kuhusu jambo pia umemfanya kupoteza ufuasi na uaminifu kutoka kwa waliomtegemea .Kando la eneo la ukambanai anakotoka ,Musyoka amekosa kujenga mtandao ya kitaifa wa uungwaji mkono na hilo linaathiri pakubwa uwezo wake kujitangaza kwa njia huru bila msaada wa vigogo wengine thabiti kutoka maeneo mengine ya nchi . Ripoti kwamba Kivutha KIbwana na Alfred Mutua wanazingatiwa kama wagombeaji wa urais kutokea eneo la Ukambani pia ni mambo ambayo yamemfanya Kalonzo kuwekwa nyuma ya fikra za waliomzingatia kama kigogo ajaye anayeweza kuiongoza nchi . Maajuzi katika utawala wa rais Kenyatta ,kalonzo amevuruga hata zaidi taadhima yake alipojitangaza kuwa ‘mtu wa mkono wa rais kenyatta’.Matamshi hayo yaliwashangaza wakaazi wa ngome yake wasijue iwapo kigogo wao amesalimu amri au yungali anataka kuwa mfalme .Amekuwa mgobea mwenza wa Raila mara mbili katika uchaguzi wa 2013 na 2017 lakini wengi wanafahamu hawakuaminiana na uhusiano huo ulikuwa tu wa kuweza kushughulikia uchaguzi .Kwa sasa haijulikani mkakati wake ni upi ,iwapo atawania urais ama atajiunga na mojawapo ya makundi makuu yatakayoibuka ili kupewa nafasi katika serikali itakayoundwa na mshindi .
5.Fred Matiang’i
Miaka saba iliyopita hungeweza kufahamu kwamba Fred Matiang’i angekuwa katikati ya kitovu cha utawala wa serikali ya Jubilee . uchapakazi wa waziri huyu wa usalama wa ndani umempepeza hadi kilele cha usimamizi na utawala wa shughuli za kila siku za serikali ya rais Uhuru kenyatta .unasposkia msemo ‘mkono wa serikali’ basi mkono huo ni wa Matiang’i. Sio ajabu basi kwamba kuna mnong’ono kwamba waziri Matiang’I huenda akagombea urais mwaka wa 2022 kwa msingi wa utendakazi wake na nidhamu ambayo ameivuta katika wizara amabazo ameziongoza tangu alipoteuliwa kuwa waziri wa ICT katika muhula wa kwanza wa rais Kenyatta . Mageuzi yamefanyika katika kila wizara hizo ikiwemo ya elimu alipokabioliana na zimwi la udanganyifu wa mitihani ya kitaifa na sasa katika wizara ya usalama wa ndani . Ili kuondoa machoni orodha ya wanasiasa wanaogombea kiti hicho ,huenda Matiang’i au wandani wake waliomjenga wakampepeza hadi katika kilele cha kampeini za kuitwaa afisi ya juu zaidi ya uongozi wa taifa .Pia kuna uvumi kwaba endapo hatowania urais ,Matiang’I ni kiungo muhimu sana katika tiketi ya urais na huenda akavutia sana kama mgombea mwenza .Ni semi tu ambazo haziwezi kuaminika wala kupuuzwa lakini siasa zina marefu yake .Pia kuna hofu kuhusu hatma yake kama mojawapo ya watu wenye ushawishi mkubwa serikalini ambayo baadaye walitokomea kwa majuto na njia za kuhurumisha .
6.Alfred Mutua
Msemaji huyu wa zamani wa serikali aliweza kuitumia nafasi hiyo kujipa umaarufu na wakati mwafaka ulipowadia ,akatumia thamani ya umaarufu wake kuwa gavana wa Machakos .Kwa mihula miwili ameiongoza kaunti hiyo na kuweza pia kujitangaza kama chaguo mbadala kwa kalonzo musyoka katika kutoa mwelekeo wa kisiasa kwa jamii ya wakamba . Alfred Mutua ,ametangza kwamba atawania urais na kama mtaalam wa kusema huwezi kumpuuza kwa sababu anafahamu fika mbinu zote za kumshawishi yeyote .Swali ni je,Mutua ana uwezo wa kuwashawishi vigogo na mabwenyenye tajika nchini kumpa jeki ya kuwania na kushinda urais? Iwapo Daktari atafaulu kufanya hilo kasha ajipate katika orodha ya vigogo wanaoweza kumpa ushindani wa kutosha naibu wa rais William Ruto basi huenda akawa na fursa ingawa matokeo yake hayawezi kutabirika kwa sasa .Kupata uongozi wa aina yoyote hihitaji ukakamvu wa aina Fulani na mkusanyiko wa mambo mengi ikiwemo bahati .Alfred Mutua huenda akajipata katika wakati mzuri katika hali ifaayo ili kukipata kiti hicho au kuchangia pakubwa mtu mwingine kushinda urais .
7.Moses Wetangula
Kiongozi huyo wa Ford Kenya na Seneta wa Bungoma hajawahi kuwania urais lakini wimbo wake umekuwa kwamba lazima atawania kiti hicho mwaka wa 2022 . Iwapo Wetangula ana ushawishi wa kutosha kupata kora za magharibi katika kapu moja ,ni jambo linalofaa kujadiliwa lakini mambo yalivyo sasa ,itahitaji mambo mengi kubadilisha kwa njia ya haraka sana kumpepeza katika nafasi ya kuweza kabisa kuwatoishia wagombeaji wengine kushinda kiti hicho.Wetang’ula anasalia kuwa katika kundi la viongozi wanaoweza kushinda kiti cha urais baada ya maafikiano ya kabla ya kura ili kuungwa mkono .kama mwanasiasa kivyake ,wakati huu na itakapofika 2022 Wetangula hana uwezo wala hadhi ya kuweza kunyakuwa ushindi wa kuingia Ikulu bila usaidi mkubwa sana kutoka kwa vigogo wa kisiasa kutoka sehemu mbali mbali za taifa.
8.Wycliffe Oparanya
Gavana huyo wa Kakamega anayekamilisha muhula wake wa Pili ,amesema kamwe mkondo wake wa siasa ni kuelekea katika siasa za kitaifa .Wadadisi wanasema Oparanya ana fursa nzuri sana ya kuweza kuwa rais endapo viongozi wengine wa magharibi watamwunga mkono na kuweka kura zote za magharibi katika kapu moja . Umaarufu wake pia umepigwa jeki na hatua nzuri za kimaendelea alizopiga katika kaunti ya Kakamega katika miaka 7 kama gavana . Endapo kweli lengo lake ni kuwania na kushinda urais mwaka wa 2022 ,Oparanya kwanza anafaa kuwashawishi wenzake wa magharibi kama vile Eugene Wamalwa ,Musalia Mudavadi na Moses Wetangula kumwunga mkono . Thamani yake kubwa hata hivyo kabla ya chochote kubadilika tunapoelekea uchaguzi mkuu wa 2022 ,ni kuimarisha tiketi ya mgombea mkuu wa urais kama mgombea mwenza.