• Mbunge wa Starehe Charles Njagua hii leo amefanya ziara katika soko la Gikomba ambapo amekutana na wafanyibiashara ambao walipoteza mali yao kwa moto uliopelekea hasara ya mamilioni ya pesa.
• Ameahidi wafanyibiashara kuwa chama cha UDA kitapigania masilahi yao.
• Mbunge huyo anaamini atashinda kiti hicho kwa mara ya pili mtawalia.
Mbunge wa Starehe Charles Njagua siku ya Jumatano amefanya ziara katika soko la Gikomba ambapo amekutana na wafanyibiashara ambao walipoteza mali yao kwa moto uliopelekea hasara ya mamilioni ya pesa.
Akiwa katika harakati hiyo, mbunge huyo amekutana na wachuuzi wengine katikati mwa jiji la Nairobi ambapo ametoa ahadi kwamba atahakikisha wafanyibiashara wote katika eneo hilo wamepata mazingira faafu ya kufanikisha shughuli zao za kutafuta hela.
Siasa za "bottom-up" zilisheheni mkutano huo, huku Jaguar akipigia debe hatua yake ya kuingia katika chama cha UDA kinachoongozwa na naibu rais William Ruto, akisema kwamba ndicho chama pekee ambacho kitashughulikia masilahi yao na kuboresha hali zao kimaisha.
Njagua ambaye katika uchaguzi uliopita alishinda uchaguzi kupitia tikiti ya chama cha Jubilee, mwaka huu atakuwa anawania wadhifa huo wa eneo bunge la Starehe kupitia chama cha UDA, kujaribu bahati yake kwa awamu ya pili mtawalia.