Kiambu: Mtoto wa miaka 10 avamiwa na kuliwa na fisi hadi kufa

Kulingana na wakazi, wavulana hao walikimbia kuokoa maisha yao walipovamiwa na mmoja wao kuanguka na kuuawa na wanyama hao wa porini.

Muhtasari

• Kulingana na wakazi, wavulana hao walikimbia kuokoa maisha yao walipovamiwa na mmoja wao kuanguka na kuuawa na wanyama hao wa porini. 

• Mabaki ya kijana huyo yalipatikana Jumapili asubuhi. Nguo zake zilizokuwa na damu zilipatikana na wafanyakazi wa machimbo katika kichaka kilicho karibu.

FISI
FISI
Image: HISANI

Wakaazi wa eneo la Witeithie, Juja, kaunti ya Kiambu walibaki na mshangao wikendi baada ya kundi la fisi kumuua mtoto wa miaka 10.

Mvulana huyo alikuwa mwanafunzi wa darasa la nne katika Shule ya Msingi ya Highway na inasemekana alikuwa akitembea nyumbani na marafiki zake Jumamosi jioni walipovamiwa na wanyama hao.

Mabaki ya kijana huyo yalipatikana Jumapili asubuhi. Nguo zake zilizokuwa na damu zilipatikana na wafanyakazi wa machimbo katika kichaka kilicho karibu.

Wakazi wa eneo hilo wanasema sasa wanaishi kwa hofu na hawawezi tena kutembea usiku.  Ripoti zinasema kuwa fisi watatu walionekana Jumamosi wakirandaranda katika kijiji hicho.

Wakiwa na wasiwasi kwamba maafisa wa Huduma ya Wanyamapori nchini (KWS) wameonyesha uvivu katika  kudhibiti hali hiyo licha ya maombi mengi, wenyeji wanaomba uingiliaji kati wa haraka ili kuepusha mgogoro zaidi.

Mashambulizi kama haya ni ya kawaida katika eneo hilo. Mwaka jana mnamo Septemba, mvulana wa miaka tisa aliuawa kwa kukatwakatwa na kundi la fisi.

Kisa hicho kimejiri miezi michache tu baada ya mwanamume mwenye umri wa miaka 35 kutoka kijiji jirani cha Athi pia kushambuliwa kwa mtindo sawia na takriban fisi wanane.

Hapo awali, watu wawili zaidi walikuwa wameshambuliwa na wanyama hao katika kijiji cha Witeithie Juja na eneo bunge la Thika mtawalia.