Watu 24 wameuawa, 32 wametekwa nyara wakati wa maandamano-Amnesty International

Shirika hilo lililaani matumizi ya nguvu ya polisi kupita kiasi dhidi ya timu za dharura na waandishi wa habari.

Muhtasari
  • Aidha waliitaka serikali kuzingatia matakwa yaliyotolewa na vijana wa Kenya ikiwa ni pamoja na kuachiliwa kwa wale waliozuiliwa na mamlaka ya polisi na kuwajibika katika utawala.

Wakenya 24 wamethibitishwa kufariki dunia Jumapili usiku kutokana na ukatili wa polisi katika maandamano ya hivi majuzi nchini kote, shirika la Amnesty International limesema.

Katika taarifa siku ya Jumatatu, shirika hilo la kutetea haki za binadamu lilisema kuwa aliyepoteza maisha ni mtoto wa miaka kumi na miwili aliyetambulika kama Kennedy Onyango.

Zaidi ya hayo, watu 361 wamejeruhiwa, 627 wamekamatwa na utekaji nyara 32 uliofanywa tangu mwanzo wa harakati za kupinga Muswada wa Sheria ya Fedha 2024 na maandamano dhidi ya serikali mnamo Juni 18.

"Kutekwa nyara na kuwekwa kizuizini kunatofautiana na kukamatwa. Wengi wa waliotekwa nyara na maafisa wa serikali hawakusomewa mashtaka dhidi yao au kupelekwa katika kituo cha polisi. Makumi wameshikiliwa kwa siri na kunyimwa fursa ya kuonana na familia zao, uwakilishi wa kisheria na msaada wa matibabu," Amnesty ilisema.

Shirika hilo lililaani matumizi ya nguvu ya polisi kupita kiasi dhidi ya timu za dharura na waandishi wa habari.

"Wahudumu wa afya wameshutumiwa, wakikamatwa na maafisa wa serikali na kuibiwa orodha zao za wagonjwa kutoka kwenye vituo vya dharura vilivyohudumia waliojeruhiwa.

Mawakili wamenyimwa nafasi ya kuwafikia wateja wao, kukamatwa, na kutishwa na maafisa wa serikali kufuta kesi," Amnesty ilisema. "Waandishi wa habari wanaoripoti maandamano hayo wamenyang'anywa kamera zao, kukamatwa na kupigwa mchana kweupe.

Aidha waliitaka serikali kuzingatia matakwa yaliyotolewa na vijana wa Kenya ikiwa ni pamoja na kuachiliwa kwa wale waliozuiliwa na mamlaka ya polisi na kuwajibika katika utawala.