Rais Ruto ampongeza Kagame kwa kuchaguliwa tena kama Rais Rwanda

Kagame amekuwa Rais wa Rwanda tangu mwaka 2000.

Muhtasari

•Ruto alithibitisha dhamira ya Kenya ya kuendelea kufanya kazi kwa karibu na Rwanda kwa manufaa ya raia wa nchi hizo mbili.

•Kagame alichaguliwa tena kuwa rais wa Rwanda kwa muhula wa nne kwa ushindi wa kishindo.

Rais Ruto wasalimiana na Rais Kagameh
Image: HISANI

Rais William Ruto wa Kenya amempongeza  Paul Kagame kwa kuchaguliwa tena kama Rais wa Rwanda.

Ruto alitoa pongezi hiyo kwa niaba ya wananchi na Serikali ya Kenya, akimpongeza Kagame kwa muda mwingine wa kuongoza nchi ya Rwanda.

"Tunasherehekea pamoja nawe chaguo la uhuru la wananchi wa Rwanda na tunakutakia mafanikio katika kuendelea kuiongoza nchi yako katika njia ya amani, utulivu, na ustawi," Ruto alisema.

Aliongeza matumaini yake kwamba Rwanda itaendelea kufikia maendeleo makubwa chini ya uongozi wa Kagame.

Ruto alithibitisha dhamira ya Kenya ya kuendelea kufanya kazi kwa karibu na Rwanda kwa manufaa ya raia wa nchi hizo mbili.

"Natarajia kuendelea kufanya kazi nawe katika masuala ya kikanda na Afrika nzima katika kudumisha uhusiano imara na umoja kati ya watu wa Kenya na Rwanda," Ruto alihitimisha.

Kagame alichaguliwa tena kuwa rais wa Rwanda kwa muhula wa nne kwa ushindi wa kishindo.

Katika matokeo ya sehemu yaliyotolewa na Tume ya Uchaguzi Taifa, Rwanda, Kagame alikuwa akiongoza katika uchaguzi uliofanyika Jumatatu.

Tume ilisema Kagame ana kura 7,099,810 ambayo ni asilimia 99.15 ya kura zote zilizohesabiwa.

Katika matokeo ya sehemu, mpinzani wake wa karibu, Habineza Frank alikuwa na kura 38,301 huku Mfayimana Philippe akiwa wa mwisho na kura 22,753.

Kagame amekuwa Rais wa Rwanda tangu mwaka 2000.

Kiongozi huyo amekuwa mamlakani katika siasa za Rwanda tangu vikosi vyake vilipochukua madaraka mwishoni mwa mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 ambayo yalisababisha vifo vya watu takriban 800,000 wa kabila la Watutsi na Wahutu.

Ametawala katika kila uchaguzi tangu kuwa Rais mwaka 2000, akishinda zaidi ya asilimia 90 ya kura.

Mwaka 2017, alishinda kwa asilimia 99 ya kura.