Shida yangu na Uhuru ni kutowania muhula wa 3, tungeshinda! - Mwanawe Museveni, Muhoozi

Kainerugaba alisema kuwa wamezungumza na Uhuru Kenyatta na hivi karibuni atazuru Uganda

Muhtasari

• Nimeongea na kaka yangu mkubwa, Afande Uhuru. Mtu wa ajabu! Atazuru Uganda hivi karibuni - Muhoozi Kainerugaba.

Muhoozi Kenyatta asema ana tatizo na Uhuru Kenyatta kwa kutowania muhula wa tatu
Muhoozi Kenyatta asema ana tatizo na Uhuru Kenyatta kwa kutowania muhula wa tatu
Image: PSCU

Muhoozi Kainerugaba ambaye ni mtoto wa rais wa Uganda Yoweri Museveni amezua gumzo kubwa nchini Kenya baada ya kudai kwamba ana tatizo kubwa na rais mstaafu Uhuru Kenyatta kwa kutowania awamu ya tatu kama rais.

Kupitia ukurasa wake wa Tweeter, jenerali huyo mkuu wa majeshi ya Uganda alidokeza kwamba Uhuru Kenyatta kutowania kwa awamu ya tatu kuliwakosesha watu wengi nafasi, akiwemo yeye mwenyewe kama mtoto wa Museveni.

“Shida yangu pekee na kaka yangu mkubwa mpendwa (Uhuru Kenyatta) ni kwamba hakugombea muhula wa tatu. Tungeshinda kirahisi!” Muhoozi Kainerugaba aliandika.

Aliweka wazi kuwa tayari amekuwa na mazungumzo ya kina na rais huyo mstaafu wa Kenya na kwamba hivi karibuni atatembelea taifa la Uganda kwa mazungumzo ya kina zaidi.

“Nimeongea na kaka yangu mkubwa, Afande Uhuru. Mtu wa ajabu! Ninampenda kwa ujasiri wake, uaminifu na akili! Atazuru Uganda hivi karibuni,” Muhoozi alisema.

Ikumbukwe Muhoozi amekuwa akitajwa mara si moja kuwa ndiye mtu ambaye rais Museveni ambaye ni babake anazidi kumkuza na kumlea kama mrithi wake kama rais wa Uganda pindi atakapostaafu.

Museveni ni mwandani mkubwa sana wa rais wa sasa wa Kenya William Ruto na matamshi haya ya mwanawe yanaonekana kutia doa katika urafiki wa babake na rais Ruto, katika kile ambacho wengi wanahisi Kainerugaba anataka uongozi wa babake pasi na kupitia mchakato wa kushiriki uchaguzi kwa kuhofia vishindo vya kasi ya ajabu kutoka upinzani ukiongozwa na Bobi Wine.