Tweet zangu ziliwaogopesha Wakenya kupita kiasi - Muhoozi Kainerugaba

KOT, nawasamehe wote kwa matusi mliyonitusi - Muhoozi Kainerugaba.

Muhtasari

• Awali alikubali kushindwa na kusema amewasamehe Wakenya kwenye Tweeter kwa kumtupia maneno yasiyonakilika.

Kainerugaba asema Tweet zake ziliwatia woga sana Wakenya
Kainerugaba asema Tweet zake ziliwatia woga sana Wakenya
Image: Tweeter

Jioni ya Jumatatu jenerali mkuu wa majeshi ya Uganda Muhoozi Kainerugaba ambaye pia ni mtoto wa rais Yoweri Museveni aligonga vichwa vya habari nchini Kenya baada ya kuachia maneno kwenye Twitter yake akiichokoza Kenya.

Kainerugaba alisema kwamba akiamua kuanzisha vita baina ya jeshi la Uganda na Kenya, haitawachukua zaidi ya wiki mbili kuteka jiji kuu la Kenya – Nairobi.

Wakenya hawakufurahishwa na matamshi haya ambapo waliamua kufanya kile ambacho wanakifanya kwa ufasaha – kuanzisha vita vya maneno na Waganda.

Mpaka asubuhi ya Jumanne, bado wakenya na Waganda walikuwa wamekunjiana mashati kwenye mtandao wa Tweeter huku wakirushiana cheche kali za kubezana.

Kainerugaba ambaye ndiye chanzo cha mgogoro huu alirudi tena kwenye Tweeter yake na kuonekana kuinua mikono baada ya Wakenya kumtupia mabomu moto. Kainerugaba aliwasihi Wakenya kukoma kuendeleza ugomvi huo na badala yake kuungana kufanya kazi kwa pamoja.

“KOT, nawasamehe wote kwa matusi mliyonitusi. Tafadhali tushirikiane kuifanya Afrika Mashariki kuwa kubwa!!!” Kamanda huyo wa majeshi ya Uganda aliandika.

Pia alidokeza kuwa amefanya mazungumzo na babake ambaye ni rais Yoweri Museveni na hata kuweka wazi kuwa alishangaa matamshi yake yaliwatia woga sana Wakenya ambao waliamua kujibu mipigo Tweeter kwa vita vya maneno.

“Nilikuwa na mazungumzo mazuri na baba yangu mkubwa asubuhi ya leo. Inaonekana, tweets zangu ziliwaogopesha Wakenya kupita kiasi? Atatangaza mabadiliko. Kuna maombi maalum nitafanya kwa ajili ya jeshi letu,” Kainerugaba alisema.

Katika Tweet za Jumanne, Kainerugaba alionekana kudokeza kunyenyekea na hata kutoa jumbe za kutaka kuunganisha mataifa ya Afrika Mashariki hata zaidi huku akisema kuwa wa wao kama viongozi wachanga katika ukandaa huu ni sharti wavunje mipaka iliyowekwa na Wakoloni na kufanya kazi kwa pamoja kama ndugu.